The House of Favourite Newspapers

Kimbunga Chaua 3 Comoro, Chaelekea Msumbiji/Tanzania

 

KIMBUNGA Kenneth kinachovuma katika Bahari ya Hindi kusini-mashariki mwa Afrika,  kimesababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu katika visiwa vya Comoro.

 

Taasisi ya kitaifa ya utabiri wa hali ya hewa ya Msumbiji (INAM) inaeleza kwamba kimbunga kimefikia kiwango cha tatu cha nguvu za vimbunga na kutabiri kitapata nguvu zaidi kabla ya kuwasili nchi kavu na kufikia kiwango cha 4. Upepo mkali ulioambatana na mvua umesababisha maporomoko ya ardhi katika kisiwa kikuu cha Ngazija.

 

Hakuna habari za majeruhi na mkuu wa idara ya huduma za dharura, Mwinyi Daho, ameliambia shirika la habari la AFP kwamba ni vigumu kwa hivi sasa kujua kiwango cha uharibifu kutokana na barabara nyingi kuharibiwa na hakuna umeme katika kisiwa chote.

 

Inaripotiwa kwamba maelfu ya watu wamepoteza makazi na ni vigumu kufika katika maeneo yaliyoathirika zaidi kiswani Ngazija.

 

 

Kimbunga hicho kinatazamiwa kuwasili kwenye pwani ya kusini mwa Tanzania na kaskazini mwa Msumbiji usiku wa Alhamisi ikiwa kitaendelea na kasi na mwenendo wake wa hivi sasa kulingana na watabiri wa hali ya hewa.

 

Ni mwezi mmoja umepita tangu  kutokea kwa Kimbunga Idai kilichosababisha hasara kubwa na vifo huko Msumbiji, Zimbabwe na Malawi.

 

 

Idai kilisababisha vifo vya watu wapatao elfu moja na hasara ya mali yenye thamani ya Dola bilioni 2 kwa mujibu wa Benki Kuu ya Dunia.

Taasisi ya kitaifa ya utabiri wa hali ya hewa ya Msumbiji INAM inaonya kwamba kimbunga Kenneth kinazidi kupata nguvu na kutahadharisha kwamba watu 692,000 wanaweza kuathiriwa kutokana na upepo huo mkali na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha.

 

Comments are closed.