The House of Favourite Newspapers

Kisa Binti Yake, Afande Amwaga Machozi ‘Sina Mpango wa Kuoa’

MACHOZI ya furaha yamemmwagika mkongwe muziki wa Bongo Fleva, Seleman Msindi almaarufu kwa jina la ‘Afande Sele’ baada ya ndoto yake ya muda mrefu dhidi ya mwanye Tundajema ‘Tunda’ kuchaguliwa kujiunga na masomo ya Chuo Kikuu kutimia.

 

Mfalme huyo wa Mistari nchini alimwaga chozi hilo la furaha kwenye sherehe ya kumpongeza Tunda kuchaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu Cha Kilimo Cha Sokoine ‘SUA’ kilichopo mkoani Morogoro, baada ya kuhitimu masomo ya Kidato cha Sita katika Shule ya Sekondari Kiteto iliyopo Mkoani Manyara ambapo.

 

Ndoto ya Afande Sele ilikuwa ni kumsomesha binti yake huyo mpaka Chuo Kikuu ambapo ni sehemu ya mashairi katika wimbo wake wa Karata Dume ambapo kuna msitari aliimba’ Mwanangu Tunda atasoma mpaka amalize vyuo vikuu vyote’.

 

Katika hafla hiyo ambayo ilihudhuriwa na marafiki mbali mbali wa Afande Sele akiwemo mwandishi wa Global Publishers mkoani Morogoro, ndugu wa mzazi mwenzake na Afande Sele, marehemu Asha huku beberu la mbuzi likiangushwa na watu kula na kunywa mpaka kukacha.

 

“Namshukuru sana Mungu kwa hatua hii ambayo ilikuwa ni ndoto yangu mwanangu afike Chuo Kikuu na leo ndoto hiyo imetimia ninafuraha sana ndio maana nikaamua nifanye serehe ya kumpongeza.

 

 

“Najivumia watoto wangu wawili Tundajema na mdogo wake Asantesanaa, naamini ili kumuenzi mama yao natakiwa niwasomeshe hadi mwisho, sasa Tunda anaingia Chuo Kikuu na mdogo wake yuko darasa la Pili, nitaendelea kupambana ili naye afike chuo kikuu,” alisema Afande Sele.

 

Alipoulizwa kuhusu kutafuta mwenzi mwingine baada ya mkewe kufariki dunia miaka 5 iliyopita, Afande alikuwa na hili la kujibu;.

 

“Kiukweli tangu mzazi mwenzangu Mama Tunda afariki duania sijaoa na sina mpango wa kuoa mwanamke mwingine kwa sasa, ingawa mazingira yanaturadhimisha kufanya hivyo, lakini kipaumbele changu kwa sasa ni kuwasomesha hawa watoto zangu wawili pekee niliyoachiwa na marehemu mke wangu,” alisema Afande kwa sauti ya unyonge.

 

Sherehe hiyo iliyofanyika kwenye moja ya ukumbi uliopo katikati ya Mji wa Morogoro ilisindikizwa na burudani mbali mbali zikiwemo za muziki wa live kutoka kwa mkali wa kinanda nchini Mussa Mishe Mishe, Disko kali kutoka kwa Dj Maarufu mkaani Morogoro Dj Ramso.

 

Afande Sele na mwanaye Tunda walipamba jukwaa kwa kupafomu pamoja wimbo wa Karata Dume.

 

Kwa upande wake Tunda alisema; “Kipekee namshukuru Mungu kwa hatua hii pamoja na baba yangu ambaye pamoja na kuondokewa na mpendwa mama yetu bado ametuthamini mimi na madogo wangu kwa kutupa huduma zote muhimu ikiwemo elimu.”

Na Dunstan Shekidele, Morogoro.

Comments are closed.