Kisa Waarabu, Ridhiwani Amvaa Manara
MWANACHAMA wa Klabu ya Yanga na Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete amemvaa Ofisa Habari wa Klabu ya Simba, Haji Manara kwa kumtaka aache siasa kuelekea katika mechi yao dhidi ya JS Saoura ya Algeria na badala yake asubirie dakika 90 ziamue.
Simba inatarajiwa kushuka dimbani kesho Jumamosi kuvaana na SJ Saoura ya Algeria timu ambayo anachezea Mtanzania, Thomas Ulimwengu, wakikutana katika mchezo wa awali wa Hatua ya Makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Ridhiwani alisema kuwa Simba ipunguze siasa kuelekea mchezo huu kwa kumtaka Manara apunguze kuzungumza sana na badala yake asubiri matokeo uwanjani na kuwataka wajiandae ipasavyo kuhakikisha wanaibuka na ushindi kuelekea mchezo huo kwa kuwa ndiyo wawakilishi pekee hapa Bongo.
“Nawatakia Simba kila la kheri kuweza kupata matokeo mazuri na kushinda mechi yao ya Jumamosi kwani wao ndiyo wawakilishi wetu pekee ambao wamebakia kwa sasa katika michuano ya kimataifa.
“Kwanza kabisa naomba wapunguze siasa kuelekea mchezo huu, Manara amekuwa akizungumza sana kupitia mitandao ya kijamii hivyo ni vyema akaacha kuongea sana na badala yake asubiri mechi ichezwe na timu iweze kujiandaa vyema kuelekea katika mchezo huo.
“Jambo lingine ambalo nimependa kuwashauri Simba ni katika suala hili la viingilio ambapo kuna kiingilio cha shilingi laki moja huku wenye magari yao watatakiwa kuacha hotelini, jambo hili si sahihi siyo watu wote wenye kiasi hicho cha fedha cha kuweza kutoa ili kuingia uwanjani.
“Wawaache watu waingie uwanjani wakafurahie mpira kama ilivyokuwa katika michezo iliyopita ikiwemo dhidi ya Nkana ya Zambia watu waliingia wengi na walifurahia, siyo hivyo wanavyotaka kufanya, utaratibu kama huo wenzetu Ulaya wanaufanya shabiki ananunua tiketi kwa mwaka mzima.
“Waache kufanya maamuzi ya kukurupuka, uwanjani siku zote hakuna viti vya VIP na badala yake kuna viti vya watazamaji, walizingatie hilo ili kupata mashabiki wengi watakaokwenda kuishangilia timu yao,” alisema Ridhiwani.
Stori na Khadija Mngwai
Comments are closed.