KISUTU: RCO, ILALA AULIZWA KAMA ANAPAFAHAMU ANAPOISHI RAIS MAGUFULI
MKUU wa Upelelezi Wilaya ya Ilala (RCO), Davis Msangi ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa hajawahi kumuhoji Rais Dkt. John Joseph Magufuli jinsi anavyojisikia kuhusu maneno yaliyotamkwa na mbunge wa Kawe Halima Mdee dhidi yake.
Msangi ameyaeleza hayo leo mahakamani hapo wakati akitoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba alipokuwa akijibu swali la Wakili wa utetezi, Peter Kibatala.
Katika kesi hiyo, Mdee anakabiliwa na shtaka la kutoa lugha ya uchochezi’ ‘Chafu’ kwa Rais Magufuli.
Akimuhoji shahidi huyo, Wakili Kibatala alimuuliza Msangi kama anamfahamu Rais Magufuli na anaishi wapi. Ambapo alijibu kuwa anaishi Ikulu akamuuliza tena shahidi huyo kama aliwahi kwenda kumuhoji jinsi anavyojisikia kuhusu maneno yanayodaiwa kutamkwa na Mdee kwa sababu yeye ndiye muhanga.
Msangi akijibu swali hilo aliieleza kwamba hajawahi kwenda kumuhoji wala hakutumia taratibu zozote za kumuhoji.
Msangi akiendelea kueleza katika ushahidi wake amedai kuwa hafahamu msimamo wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusiana na kauli ya Rais Magufuli kuhusu watoto wa kike waliopata mimba shule wasirudishwe shule.
Pia RCO Msangi alipoulizwa kwamba Mdee alikaa muda gani chini ya ulinzi, amedai kwamba siyo kwa zaidi ya Saa 48.
Baada ya shahidi huyo kumaliza kuhojiwa na Wakili Kibatala, Hakimu Simba amesema kesi hiyo imetimiza mwaka mmoja na ilipaswa iwe ishatolewa hukumu, na hivyo akaiahirisha kesi hiyo hadi Agosti 7 mwaka huu ili kuendelea na ushahidi.
Comments are closed.