The House of Favourite Newspapers

KITALE NOMA! AWAJIBU JOTI, MASANJA KWA MJENGO WA MAANA

BAADA ya maneno mengi kuwa tasnia ya filamu Bongo hailipi, staa wa vichekesho, Yusuph Mussa Kitale ‘Mkude Simba’ au Rais wa Mateja’ ameangusha mjengo wa maana na kuondoa kabisa mawazo kwamba tasnia hiyo hailipi. 

Hadi hapo ulipofikia kabla ya finishing (kumalizika kabisa), mjengo huo umegharimu kiasi cha shilingi milioni 78.

 

Kitale anayerusha vichekesho vyake kupitia Radio EFM amewajibu mastaa wa vichekesho wanaotamba kwa mijengo mikali Bongo kama Lucas Mhuvile ‘Joti’ na Emmanuel Mgaya ‘Masanja Mkandamizaji’. Kama ilivyo kwa Joti na Masanja, mjengo wa Kitale nao upo Kigamboni, eneo la Kibada jijini Dar.

 

Joti na Masanja wanamiliki mijengo ya kifahari ya ghorofa mojamoja maeneo ya Kigamboni jijini Dar. Akizungumza na Gazeti la Ijumaa Wikienda juu ya mjengo huo, Kitale alisema anatarajia kuhamia kwenye mjengo huo mara tu utakapomalizika kwa kuwa upo katika hatua za mwisho.

“Nitahamia mara tu nitakapomaliza kuujenga maana upo katika hatua za mwisho na umegharimu kiasi cha shilingi milioni 78 za Kitanzania.

 

“Sanaa ambayo ninafanya (uigizaji wa vichekesho) ndiyo imeniwezesha kujenga kwani sina kipato kingine zaidi ya sanaa ila kikubwa ni kuweka malengo na ukiweka malengo ya kufanya kitu na ukaweka nia pia utafanikiwa.

“Ninachojua mimi hakuna pesa ndogo kama utaifanyia kile ambacho umekusudia.

“Kwa hiyo mimi kwa upande wangu sanaa inalipa na ndiyo maana nimefanya hivi na natarajia kufanya vitu vikubwa zaidi. Kipaji changu ni sanaa, ninafanya kwa kadiri ambavyo itaniletea manufaa,” alisema Kitale ambaye pia amefanya filamu nyingi za vichekesho kama Chizi Kalogwa Tena, Simu ya Kichina, Bwege Mtozeni nk.

Comments are closed.