Kiungo Simba Apeleka Mkataba Yanga SC
KIUNGO mchezeshaji fundi wa Simba, Mohammed Ibrahim amesema kuwa yupo tayari kujiunga na Yanga kwenye msimu ujao kama wakihitaji saini yake.
Nyota huyo anayekipiga kwa mkopo Namungo FC ya Lindi, ni kati ya wachezaji ambao mikataba yao inatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu huu.
Mastaa wengine wanaomaliza mikataba yao Simba ni Yusuph Mlipili, Pascal Wawa, Sharraf Shiboub, Deo Kanda na Hassani Dilunga wanaotarajiwa kuongezewa mikataba.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Mo alisema kuwa tayari baadhi ya klabu zimemfuata na kumpa ofa ambazo zipo kwenye majadiiliano ya dau la usajili ambalo yeye analitaka ili asaini.
Mo alisema kati ya timu ambazo zimempa ofa ni Namungo anayoichezea kwa ajili ya kumpa mkataba mrefu wa kubaki kuendelea kukipiga hapo, licha ya yeye kuwepo kwenye mipango ya kuondoka hapo. Aliongeza kuwa ni wakati muafaka wa yeye kutoka hapo na kwenda kutafuta changamoto nyingine mpya kwenye moja ya klabu ili kurejesha heshima yake iliyopotea.
“Mkataba wangu na Simba unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu huu, na kama mambo yakienda vizuri basi nitaondoka hapo na kwenda kwingine kutafuta changamoto mpya.
“Tayari baadhi ya klabu zimenifuata kwa ajili ya kufanya mazungumzo na kikubwa kujadiliana katika dau la usajili ambalo mimi ninalitaka, ni mapema kuzitaja klabu hizo, tusubirie muda muafaka ukifika itaweka wazi.
“Kikubwa nimepanga kufanya mengi makubwa katika msimu ujao kwenye klabu hiyo mpya nitakayokwenda kuichezea, hakuna asiyefahamu kiwango change, hivi sasa ninafanya mazoezi ya nguvu kwa ajili ya kujiweka fiti zaidi,” alisema Mo. Mo aliyewahi kuichezea timu ya taifa, Taifa Stars, alijiunga na Simba akitokea Mtibwa Sugar.
STORI: WilBErt molandi