Kiwanda Cha Mafuta Chaungua Moto Shinyanga, Majeruhi 4 Wakimbizwa Hospitalini
MOTO umezuka na kuteketeza sehemu ya kiwanda cha kuchakata mafuta ya kupikia yatokanayo na mbegu za pamba cha Jielong kilichopo eneo la viwanda Manispaa ya Shinyanga.
Katika ajali hiyo iliyotokea jana majira ya saa 10 jioni, wafanyakazi wanne wamejeruhiwa na walikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Shinyanga kwa matibabu zaidi.
Moja ya wafanyakazi wa kiwanda hicho, Thomas Mayunga, amesema wakati wakiendelea na majukumu yao, majira saa 10 jioni mashine moja iliingiliwa na mchanga, ndipo kukatokea msuguano na kisha moto kuanza kuwaka.
Mratibu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Shinyanga, Ramadhani Kamo amesema mara baada ya kupata taarifa majira ya saa 11, walifika katika eneo hilo na kuanza shughuli ya kuuzima moto huo.
Kamo amesema, mpaka sasa jitihada za kupata chanzo cha ajali hiyo bado zinaendelea kwa kushirikiana na wamiliki wa kiwanda hicho cha Jielong.