Kocha Awachenjia Wachezaji Simba
KIPIGO cha mabao 2-1 walichokipata kutoka kwa Bandari juzi kiliwatokea puani baada ya jana Kocha Patrick Aussems kuwaanika juani kwa zaidi ya dakika 60 walipokuwa na kikao kizito kilichofanyika kwenye Uwanja wa Boko Veterani.
Katika kikao hicho kilichoanza kabla ya mazoezi, Aussems alitumia muda huo kuwakumbusha wachezaji hao majukumu yao ambayo wanapaswa kuifanyia Simba katika kipindi hiki ambacho inakabiliwa mi mechi nyingi ngumu.
Mmoja wa wachezaji wa Simba ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini aliliambia Spoti Xtra kuwa: “Mbali na kutukumbusha majukumu yetu lakini pia kocha alizungumzia kuhusiana na kiwango kibovu tulichoonyesha tulipocheza na Bandari juzi Ijumaa.”
“Alisema hakufurahishwa kabisa na uwezo wetu tulioonyesha katika mechi hiyo, kwa hiyo ametutaka tujitambue na kuachana na tabia ya kuweka mbele starehe kuliko kazi.
Katika hatua nyingine, msemaji wa klabu ya Simba, Haji Manara amewaomba radhi mashabiki kufuatia kutolewa kwa timu yao kwenye michuano ya Sportpesa.
Manara alisema wanaelewa fika kuwa mashabiki wameumizwa na kutolewa huko kwa timu yao kwa hiyo amewaomba watulie huku kocha akirekebisha makosa ili wafanye vizuri kwenye Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika.
STORI NA SWEETBERT LUKONGE
Comments are closed.