The House of Favourite Newspapers

Kocha Simba aipa Yanga mbinu… 10… za kuwaua Waarabu

0

Wilbert Molandi,
Dar es Salaam
WAKATI ikijiandaa kuvaana na Al Ahly ya Misri, kocha na mchezaji wa zamani wa Simba, Abdallah ‘King’ Kibadeni, ameipa Yanga mbinu kumi za kuwaondoa Waarabu hao kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

Yanga itavaana na Al Ahly katika raundi ya pili ya michuano hiyo, kati ya Aprili 8 au 9, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Timu hiyo, itavaana na Al Ahly baada ya kuwatoa APR ya Rwanda kwa jumla ya mabao 3-2 huku Al Ahly ikiitoa Recreativo do Libolo ya Angola.
Akizungumza na Championi Jumatano, Kibadeni mwenye heshima kubwa kisoka Afrika, alisema Yanga ina kikosi bora na chenye ushindani, hivyo ina nafasi kubwa ya kufuzu hatua inayofuata na kikubwa inachotakiwa kukifanya ni mambo kumi kama ifuatavyo:

1.Kujiamini/maandalizi ya kutosha
“Kitu cha kwanza kabisa inachotakiwa kukifanya ni kujenga hali ya kujiamini kuwa wana timu bora itakayowatoa Waarabu hao, pia kufanya maandalizi ya kutosha kabla ya mechi hiyo ambalo ni jukumu la benchi la ufundi.

2.Wachezaji kujitambua
“Hilo nalo ndiyo jambo la msingi analotakiwa kuwa nalo kila mchezaji katika kufanikisha malengo yao ya kuwatoa Waarabu hao, hivyo kila mchezaji anatakiwa kujitambua kabla ya mchezo huo kuwa wanaingia uwanjani kufuata ushindi na siyo kitu kingine.

3.Kila mchezaji kutimiza wajibu wake
“Katika kuhakikisha Yanga wanafanikiwa kuwatoa Al Ahly, kila mchezaji anatakiwa kutimiza wajibu wake aliopewa na kocha ndani ya uwanja, ikiwemo mabeki kutoruhusu bao golini kwao, viungo kuichezesha timu na washambuliaji kufunga mabao, hilo ndilo jambo la msingi.

4.Kushambulia dakika zote 90
“Yanga inatakiwa kujitengenezea akiba ya mabao kwa kuhakikisha inashinda mechi ya nyumbani kwa idadi kubwa ya mabao kuanzia 3-0 hadi 4-0, kuwapa ugumu Al Ahly kwenye mchezo wa marudiano nyumbani kwao, lakini siyo ushindi wa bao 1-0 halafu wakategemea kuwatoa Waarabu kwao.
5.Wasikubali sare nyumbani
“Kati ya vitu ambavyo Yanga hawatakiwi kuvifanya, basi ni kuruhusu sare nyumbani kwa sababu hao Waarabu wenyewe wanapokuja kucheza ugenini, wanafuata sare na siyo kitu kingine, hivyo wasiwaige Al Ahly aina yao ya uchezaji wa pasi nyingi zisizokuwa na faida.

6.Waarabu wanafuata sare tu ugenini
“Kwa uzoefu nilionao nikiwa kama mchezaji na kocha, timu zote za Kiarabu zenyewe ugenini zinafuata sare tu na siyo kitu kingine, hivyo watakachokifanya ni kujiangusha kwa ajili ya kupoteza muda, hivyo Yanga wanatakiwa kucheza kwa nidhamu ya hali juu.

7.Kuongeza muda wa mazoezi
“Hili suala linawahusu benchi la ufundi, kikubwa wanachotakiwa ni kuongeza muda wa mazoezi kwa ajili ya kujiweka fiti kama Yanga walikuwa wanafanya mazoezi kwa saa mbili, basi waongeze hadi kufikia tatu hadi nne, kwa sababu timu za Waarabu zina fitinesi na pumzi nyingi.
8.Yanga kulinda bao ugenini
“Yanga baada ya kupata ushindi wa nyumbani, basi wanachotakiwa mechi ya ugenini wanapokwenda huko wenyewe walinde lango lao dakika zote na kama wanashambulia, basi kwa kushtukiza siyo muda wote.

9.Viungo kuwachezesha Tambwe/Ngoma
“Yanga wana safu nzuri ya ushambuliaji inayoundwa na wachezaji wenye uzoefu kama Ngoma (Donald) na Tambwe (Amissi), hao hawatakiwi kufanya kazi ya viungo ya kufuata mipira na badala yake wanatakiwa kupelekewa wao mipira ya kufunga mabao, hapa kina Thabani Kamusoko wanatakiwa kufanya kazi sana.

10.Yanga wasiridhike
“Hawatakiwi kucheza kwa kuridhika kama watapata ushindi mnono nyumbani na badala yake kupambana kama wasipoangalia kitawakuta kama kilichotokea mechi na APR, wenyewe waliingia kwa kuridhika kwa kuona wameshamaliza na kujikuta nyumbani wakitoa sare ya bao 1-1,” alisema Kibadeni ambaye kwa sasa ni mshauri wa timu ya taifa, Taifa Stars.

Leave A Reply