The House of Favourite Newspapers

Kocha Simba: Yanga Wafanye Hivi Waifunge Zesco…

 

ALIYEWAHI kuwa Kocha Mkuu wa Simba, Muingereza, Dylan Kerr, ametoa neno la ushauri kwa Yanga kuhusu wapinzani wao, Zesco United kabla ya kukutana nao katika Ligi ya Mabingwa Afrika, Agosti 14, 2019.

 

Yanga inatarajiwa kukutana na miamba hao wa Zambia katika mchezo wa hatua ya kwanza ya ligi hiyo utakaopigwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam ikiwa ni baada ya kuitupa nje Township Rollers ya Bostwana kwa mabao 2-1.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Kerr ambaye hivi sasa yupo kwao, England akiwa hana timu amewaambia Yanga ili wafanye vema wanapaswa kuwafuatilia Zesco kwa ukaribu hasa kujua aina ya mfumo wanaoutumia ili iwasaidie katika kupata matokeo mazuri.

Ameongeza kuwa, Yanga wanatakiwa kufanyia kazi mbinu za kuhakikisha wanapata mabao kuanzia mawili ya mapema ili kupunguza presha ya mchezo na kuwafanya wawe na faida ya kucheza kwa utulivu wakiwa ugenini endapo wakiibuka na ushindi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Aidha, Kerr ametuma ujumbe kwa wachezaji wa Yanga huku akimtaja Kelvin Yondani kuhakikisha anashirikiana vema na wenzake kwenye eneo la ulinzi kulinda lango lao ili wasiruhusu bao, sababu itakuwa faida kwa Zesco United kwenye mechi ya marudiano.

 

“Ni vema Yanga wakatuma wawakilishi Zambia au hata kuwafuatilia kwa karibu Zesco mitandaoni ili kujua wanapenda kutumia mfumo upi ili waweze kuwajua.

 

“Vema wakaingia na mbinu za kupata mabao ya mapema zaidi na ni vizuri wakifunga kuanzia mawili kwenda mbele maana itawapa nguvu ya kucheza bila presha na itawasaidia kuutawala mchezo wakionyesha utulivu.

 

“Unapocheza na timu kama Zesco unatakiwa uonyeshe heshima ya mchezo, kwenye safu ya ulinzi wanaye Yondani ambaye naamini kama akishirikiana vizuri na wenzake wataweza kufanya kazi nzuri ya kutoruhusu bao lolote lile,” alisema Kerr.

 

Kocha huyo amesisitiza kwa kuwataka Yanga waonyeshe juhudi zaidi kwani ndiyo timu pekee iliyosalia kwenye mashindano hayo huku akiwatakia mema wafike hatua ya robo fainali kama watani zao Simba au zaidi ya hapo.

Stori na George Mganga, Dar es Salaam

Comments are closed.