The House of Favourite Newspapers

Koffi Olomide, Ng’ombe Asiyezeeka Maini

0

Mwanamuziki, Koffi Olomide.

Andrew Carlos

MWAKA 1950, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) alitokea msanii wa muziki wa Soukous (Lingala/Rumba ya Kongo), Verkys Kiamuangana Mateta ambaye aliitetemesha Kongo akiwa na Bendi ta TPOK Jazz.

Verkys hakudumu sana kwenye Bendi ya TPOK Jazz kwani alitamani kuwa na bendi yake mwenyewe ambapo mwaka 1960 alifanikiwa kumiliki bendi ya Orchestre Vévé na haikuishia hapo, miaka kumi mbele aliongeza bendi mbili ambazo ni Orchestre Kiam na Orchestre Lipua Lipua akiwa na wanamuziki wakali kama Nyboma Mwandido pamoja na Pepe Kalle.

Miaka ya 1980, Verkys aliamua kuachana na muziki na kufanya biashara nyingine lakini akawa ameshaweka alama kubwa ya muziki huo DRC.Kuacha muziki kwa Verksy kukaibuliwa na msanii mwingine katika Jiji la Kinshasa aliyejulikana kwa jina la Papa Wemba aliyetokea Bendi ya Zaiko Langa Langa.

Baada ya kukaa na Zaiko Langa Langa kwa muda mrefu kidogo, Wemba aliamua naye kuanzisha bendi yake iliyojulikana Viva la Musica ambayo ilikuwa na vichwa vikali kama Pepe Bipoli, Petit Aziza, Kester Emeneya, Rigo Star, Syriana, Bongo Wende na Koffi Olomide.

Koffi ni nani?
Koffi Olomide ambaye ana majina kibao kama Grand Mopao, Numberi One, Mikael Jacksonee, Golden Star, Quadra Kora na mengineyo alizaliwa Ijumaa ya Julai 13, 1956 katika mji wa Kisangani, Kaskazini mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Koffi ana asili mbili yaani mama mtu wa (DRC) na baba yake ni mtu wa Sierra Leone. Jamaa alianza rasmi muziki akiwa na miaka 18 ambapo mbali na kuwa na kipaji cha kutunga na kuimba, pia alikuwa na akili za darasani hatua iliyompelekea kupata wadhamini wa kumlipia kwenda kusoma Bordeaux, Ufaransa na kufanikiwa kupata Shahada yake ya kwanza ya Biashara na Uchumi.

Mbali na shahada hiyo, pia jamaa ana shahada ya Hisabati kutoka Chuo Kikuu cha Paris, Ufaransa.
Muziki Umaarufu wake ulianzia alipokuwa na bendi ya Papa Wemba, Viva la Musica mwaka 1980 ambapo alikuwa mtunzi wa nyimbo na baadaye akawa muimbaji mkubwa.

Mwaka 1986 aliamua kuunda bendi yake mwenyewe kama ilivyokuwa kwa Papa Wemba (Viva la Musica), Verkys Kiamuangana (Orchestre Lipua Lipua) yeye bendi yake akaiita Quartier Latin iliokuwa na vichwa vikali kama vile Fele Mudogo, Sam Tshintu, Suzuki 4×4, Soleil Wanga, Fally Ipupa, Montana Kamenga, Ferre Gola na wengine kibao.
Mafanikio makubwa aliyapata mwaka 1990 hadi 1994 alipoibuka na albamu saba akiwa na bendi yake.
Albamu

Hadi sasa, Kofi ana albamu zaidi ya ishirini na tano zilizopo sokoni kama vile Affaire D’etat, Best Of Effrakata, Live a Bercy, Force De Frappe, Attentat, Droit De Veto, Golden Star, Diva, Les Prisoners Dorment na nyingine kibao.
Akimbiwa na wanamuziki wake

Miongoni mwa matukio ambayo Koffi hawezi kuyasahau maishani ni pamoja na la mwaka 1998 akiwa jijini Paris, Ufaransa alikimbiwa na wanamuziki wake karibu wote muda mfupi baada ya onesho kubwa lililofanyika katika Ukumbi wa Olympia.

Bendi yake ilisambaratika kwani baadhi ya wanamuziki waliotoka kwake walienda kuanzisha bendi zao nyingine ikiwa ni pamoja na Bendi ya Orchestra ‘Quartier Latin Academia’.

Kuonesha kuwa ng’ombe hazeeki maini, mwaka 1999, Koffi alilazimika kurudi Kongo na kuingia msituni ambapo aliibuka na vijana wadogo zaidi ya kumi na kuendeleza kuunda kundi lake lililobakiwa na wasanii wachache ambao ni Cindy na wengineo.

Mwaka 2001, Koffi aliitetemesha DRC na Afrika kwa ujumla baada ya kuibuka na Albamu ya Effrakata akiwa na wanamuziki karibia wote wapya na kuwazima wale wote waliomtoroka.

Selfie yamng’arisha zaidi
Tangu aanze muziki, Koffi hajawahi kutetereka na Oktoba, mwaka huu amerudi tena na ujio wake wa Selfie ambao umekuwa gumzo kila staa, kila kumbi za starehe na sehemu kibao.

Drogba amekua ni mmoja kati ya mastaa walioonekana kuukubalia wimbo huu baada ya kuonekana akiucheza na kuimba sehemu ya kiitikio (Ekotitéé), muda mfupi baada ya kumalizika kwa mechi.

Leave A Reply