The House of Favourite Newspapers

Kuna Uwezekano Babu Seya, Papii Kutoka Ndani ya Saa72

0

babuseyarufaa2Nguza Viking ‘Babu Seya’ na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’

Stori: Elvan Stambuli, UWAZI

DAR ES SALAAM: Hatimaye rufaa ya wanamuziki maarufu nchini, Nguza Viking ‘Babu Seya’ na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’, imesikilizwa katika Mahakama ya Haki za Binadamu Afrika (AfCPHR) jijini Arusha Machi 11, mwaka huu na sasa zimebaki saa 72 tu kujua hatima yao, yaani Machi 18, 2016, UWAZI linakupa zaidi.

Rufaa hiyo ilisikilizwa na mahakama hiyo yenye majaji 11 kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) ambapo rais wao ni Jaji Augustine Ramadhani wa Tanzania ambaye pia aliwahi kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania.

babuseyarufaa1MAJAJI WENYE SIRI MOYONI
Baadhi ya majaji waliotajwa kusikiliza rufaa hiyo na nchi zao kwenye mabano ni Ben Kioko (Kenya), Solomy Balungi Bassa (Uganda), Duncan Tambala (Malawi), Angelo Vasco Matuse (Msumbiji), Sylvain Ore (Ivory Coast), El Hadji Guisse (Senegal) na Rafaa Ben Achous (Tunisia).

KUTOKA MAHAKAMANI
Kwa mujibu wa chanzo cha uhakika kutoka katika mahakama hiyo, rufaa hiyo ilisikilizwa kwa faragha na hakuna mwandishi wa habari yeyote aliyeruhusiwa kuingia kupata mwenendo.
Chanzo kilizidi kusema kuwa rufaa ya mwanamuziki huyo na mwanaye, ilisikilizwa kwa karibu saa tatu tangu ianze na matokeo au hukumu wanayo wahusika.

SABABU ZAFICHWA
Hata hivyo, si Rais wa Mahakama ya Afrika, Jaji Ramadhani au mtu mwingine yeyote aliyeeleza sababu za kesi ya Babu Seya na mwanaye Papii Kocha isikilizwe faragha.

HATA JAJI RAMADHANI HAJUI
Wakati akichukua madaraka ya urais wa mahakama hiyo, Jaji Ramadhani alisema: “Kesi yoyote inayohusu nchi yangu mimi sitakiwi kuhudhuria kutokana na sheria zetu za mahakama hii…”
Kutokana na maneno hayo, kumezuka utata kwani haikujulikana mara moja kama wakati shauri la Babu Seya na mwanaye linasikilizwa, Jaji Ramadhani alikuwepo au la kwani rufaa ilipitiwa kwa faragha na kama alitoka nje basi itakuwa imepitiwa na majaji 10.

WATOA UAMUZI
Habari zaidi zinasema kuwa mara baada ya rufaa hiyo kupitiwa na majaji hao, shauri lao linapelekwa kwenye Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu ambako huko ndiko kutakakotolewa uamuzi ndani ya saa 72 zijazo.
WANACHODAI
Wanamuziki hao wamekata rufaa dhidi ya adhabu waliyohukumiwa mwaka 2004 ya kutumikia kifungo cha maisha jela ambapo mpaka sasa, wapo Gereza la Ukonga, Dar wakitumikia kifungo chao.
Kupitia shauri lao lililowasilishwa mahakamani na jalada lake kupewa namba 006/2015, wawili hao wanaiomba mahakama hiyo kutoa uamuzi kuwa haki zao zilikiukwa na wanaomba waachiwe huru na kulipwa fidia.
Pia wanataka mahakama hiyo iteue wataalam watakaotoa ufafanuzi wa hoja za kesi yao na kuisaidia kufikia wajibu wake.
Miongoni mwa hoja za Babu Seya na mwanaye zilizosikilizwa mahakamani hapo, ni pamoja na kwamba mwenendo wa shauri lao haukufanyika kwa kuzingatia haki, vilevile wanadai hati ya mashitaka dhidi yao ilikosewa kuandikwa tarehe ambayo tuhuma za makosa yao zilidaiwa kufanywa hivyo wakashindwa kutayarisha utetezi wao.
Pia wanadai mahakama iliyowatia hatiani, ilijielekeza katika ushahidi wa upande wa mashitaka pekee usioshirikisha ushahidi mwingine.

WANAISEMA SERIKALI
Wanadai kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia maofisa wake, ilivunja misingi ya haki za binadamu na sheria za kimataifa kwani ilivunja Ibara 1, 2, 3, 5, 7(1) b, 13 na 18 (1) ya Mkataba wa Afrika wa Ubinadamu na Haki za Binadamu.
Wanadai kwamba mashitaka dhidi yao yalitungwa na hivyo hukumu iliyotolewa haikujikita katika ushahidi wenye nguvu katika sheria.

TUKUMBUSHANE
Oktoba 12, mwaka 2003, Nguza na wanaye watatu, Mbangu, Johnson na Francis walikamatwa na kufikishwa Kituo cha Polisi cha Magomeni, Dar wakidaiwa kubaka na kulawiti watoto 9, maeneo ya Sinza Palestina, Dar.
Oktoba 16, mwaka huohuo walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu tuhuma hizo huku wakitetewa na Wakili Mabere Marando ambaye juzi hakupatikana alipotafutwa na gazeti hili ili kutoa ufafanuzi kupitia simu yake ya kiganjani.
Juni 25, 2004, Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Addy Lyamuya aliwatia hatiani Babu Seya na wanaye kwa hatia ya kubaka na kulawiti.
Januari 27, mwaka 2005, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Thomas Mihayo alitupilia mbali rufaa yao iliyokuwa ikipinga hukumu dhidi yao.
Awali mwaka 2004, baada ya kukutwa na hatia katika kesi hiyo, Babu Seya, Papii Kocha na wakili wao, Mabere Marando walikata rufaa ya pili ambayo ilitupiliwa mbali.
Mwaka 2010, waliomba tena rufaa ambayo marejeo yake yalisikilizwa na kutolewa hukumu Februari 2010. Mahakama iliridhia hukumu ya kifungo cha maisha kwa Babu Seya na Papii Kocha huku ikiwaachia huru watoto wake, Mbangu na Francis.

Leave A Reply