The House of Favourite Newspapers

Kutana na Oladee; Mjuba Anayelia Bila Mpangilio

0

KATI ya vitu vinavyopewa kipaumbele na Watanzania wengi hususan waliomo mijini, mitandao ya kijamii ni miongoni mwao. Yaani kuna baadhi ya watu wapo radhi wasile ilimradi tu hiyo pesa wajiunge bando na kuweza kuperuzi.

 

Mitandao hiyo huweza kukuza majina na kuwainua watu mbalimbali wakiwemo mastaa na hata watu wa kawaida na kufahamika kuvuka mipaka ya sehemu moja hadi nyingine.

Watu wengi ambao ni stadi katika utumiaji wa mitandao hiyo, mara nyingi huingiza stika au vichekesho kwenye mazungumzo yao ili kuyafanya yawe ya kupendeza, kufurahisha na yenye mvuto.

 

Kama wewe ni mfuatiliaji mzuri wa mitandao ya kijamii, basi utakuwa unamfahamu jamaa mmoja ambaye amekuwa akionekana kwenye picha mbalimbali akilia mno bila mpangilio; yaani analia hovyohovyo tu.

Ipo hivi, picha yenyewe ni moja tu, lakini watu wemeweza kuiunganisha kwenye picha za watu wengine na kuzua taharuki kila kukicha.

 

Kuna wakati zinamuonesha kwenye matendo mbalimbali kama akiongea na maiki huku akilia, akicheza mpira huku akilia, akiwa amepiga suti kali huku akilia, akiwa anakula bonge la msosi huku analia, akiwa na mwanamke mkali huku akilia na nyinginezo nyingi kama zinavyoonekana pichani.

Je, unamjua mjuba (jamaa) huyu ni nani? Unajua kwa nini huwa analia kiasi hicho? Gazeti la IJUMAA limechimba, linakupa stori kamili;

 

HISTORIA YAKE

Huyu jamaa anaitwa Oladee, raia wa nchini Nigeria. Ni kijana ambaye picha zake zimekuwa zikisambaa kwenye mitandao ya kijamii hasa ya WhatsApp na Instagram zikimuonesha akilia mno bila mpangilio.

Kwa sasa kijana huyu ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ilorin kilichopo nchini Nigeria ambaye anafunguka kuhusiana na kilichomsababishia kulia kiasi kile; yaani ni nini hasa kilitokea.

 

Oladee anasema tukio hilo lilitokea muongo mmoja uliopita (2010) wakati akiishi nyumbani kwa bibi yake.

Oladee anasema kipindi hicho, hali ya kiuchumi kijijini kwao ilikuwa ngumu mno ambapo hata chakula kupatikana ilikuwa ni shida.

 

Siku moja, bibi yake alimpa naira 200 (pesa za Kinigeria) ili akanunue garri (aina ya chakula) kwa siku hiyo, lakini badala ya kutumia kwa kusudi hilo, yeye na rafiki yake walitafuta njia mbadala ya kujiongezea pesa mara mbili kwa kucheza kamari (kubeti).

 

Kwa bahati mbaya kwake, aliishia kuliwa pesa zote. Kwa hiyo, kupotea kwa pesa kukamfanya kulia kwa tumaini la kwamba, wacheza kamari wenzake wangemsamehe na kumrudishia pesa. Pia, alipokumbuka kuhusu hali ya kiuchumi ya bibi yake aliyokuwa nayo, alijua kwamba hakutakuwa na chakula kwa siku mbili.

Sababu zote hizo zikamfanya kuangua kilio kwa hisia ili waweze kumhurumia, lakini haikuwa hivyo na hiyo ndiyo ikawa sababu ya yeye kudondosha machozi kiasi kile.

 

MAFANIKIO

Kutokana na picha yake kusambaa mataifa mbalimbali hususan Afrika, Oladee amesema anashangaa picha yake hiyo kuweza kupenya sehemu mbalimbali Afrika na hatimaye kujulikana. Licha ya umaarufu huo alioupata, lakini hapati faida yoyote kutokana na picha yake hiyo kusambaa. Anasema kuwa, faida wanaipata watu wenyewe tu pindi wanapotumiana picha hizo na kufurahi.

 

TUJIFUNZE

Kutokana na kutapeliwa kwenye kamari alikocheza kwa dhumuni la kuzalisha pesa mara mbili, tunapata funzo kuwa, tupende kujituma kwa kazi zilizo halali. Kwani kwa kipindi cha sasa vijana wengi wamekuwa wakipenda kucheza kamari kuliko hata kujituma kufanya kazi.

Makala: Amina Said.

Leave A Reply