Kwa heri Celina…
Brighton Masalu na Denis Mtima
BURIANI! Hatimaye mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti na Utumishi wa Umma, Celina Stephano Ompeshi Kombani umezikwa jana kijijini kwake, Mahenge, Ulanga mkoani Morogoro, kufuatia kifo chake kilichotokea huko India mwishoni mwa wiki iliyopita.
Katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam Jumatatu, ambako mwili huo uliagwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa, makada wa CCM, wawakilishi wa vyama vya upinzani na wananchi wa kawaida, walimwelezea marehemu kama mmoja wa viongozi walioacha alama iliyotukuka katika utumishi, kwa weledi na uwezo wake kiutendaji.
Anne Makinda, Spika anayemaliza muda wake, alisema uwezo wa marehemu ulisaidia kutatua baadhi ya mambo ya kiutawala ndani ya bunge na kwamba mara kadhaa walizingatia ushauri wake walipojikuta katika mahitaji.
“Hakika alikuwa na uwezo wa kipekee, siku chache kabla ya kifo chake, tulikutana hapa jijini Dar kwa ajili ya kumuomba ushauri kwenye mpango wa kukuza muundo wa bunge, alitoa mchango wake vizuri, taifa limepoteza nguvu kazi muhimu sana,” alisema Bi. Makinda.
Bi. Celina Kombani alifariki dunia Septemba 24 mwaka huu katika Hospitali ya Appollo nchini India ambako alikuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa kansa.
Kabla ya wadhifa wake wa sasa serikalini, Celina aliwahi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Tamisemi) 2008-2010, Waziri wa Katiba na Sheria, Naibu Waziri Tamisemi, Ofisa Utawala Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, Meneja wa Kiwanda cha Ngozi Morogoro na Ofisa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa.
Bwana alitoa, Bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe. Amen!