The House of Favourite Newspapers

Kwa nini upekue suruali za mumeo, si udokozi huo?

0

WAPENZI wasomaji wangu nina imani ni wazima na mnaendelea vema na shughuli za kulijenga taifa, mimi ni mzima kabisa, kwa wale wagonjwa nawaombea heri mtapona na kwa waliofikwa na misiba nawapa pole Mungu awatie nguvu.

Leo nimekuja na mada kali kidogo, ambayo nimeipata kwa msomaji baada ya kuongea naye kiukweli imenisikitisha sana kwani kama wewe ni kungwi halafu imetokea kwa mwari wako lazima uone aibu.

Kuna msomaji mmoja alinitumia ujumbe mfupi wa maneno kwenye simu yangu ukidai kuwa mke wake ana tabia ya kupekua suruali zake pamoja na pochi pale tu anapokuwa bafuni au anapotoka.

Msomaji huyo alieleza kuwa ni tabia ambayo inamkera sana kwani badala ya kujenga huwa anajikuta akikasirika na kugombana na mkewe.

Kwangu mimi kama kungwi hii imenikasirisha sana, hivi inakuwaje mwanamke unapekua suruali za mumeo, kwanza unatafuta nini, hivi je, amekupa uifue?
Kama amekupa uifue bila shaka haina tatizo kwa sababu huenda ameacha pesa na unataka kuzinusuru zisilowe.

Lakini hili la mume kwenda bafuni kuoga wewe ukaingia na kupekua kuangalia ana pesa kiasi gani siku hiyo ni tatizo kubwa.

Eti wengine wanapekua huenda wakakutana na vibarua au namba za simu au hata mipira hii si sahihi kabisa na ni uongo, wengine humchunguza mume ana pesa ngapi ili aanze malalamiko yake.

Ninavyoamini wakati huu si wa mwanaume kuweka namba za simu kwenye pochi au suruali, lazima mke atakuwa na dalili za udokozi tu.
Je, anachokupatia hakikutoshi?

Je, mume wako anachokupatia hakikutoshi mpaka umpekue na kama ameamua kukupa kiasi hicho kwa nini usiridhike kwanza kisha umuombe mkae na kuijadili hela anayotoa.
Niwakumbushe wanawake wenzangu, kumpekua mume si jambo jema kabisa na hii ni dalili ya udokozi, wanawake wengi wanaowapekua wanaume ni wale wasioolewa, sasa iweje wewe uliyewekwa ndani unafanya hivyo?

Wapo wanaume wachoyo kweli
Huenda mumeo ni mchoyo kweli anakupa hela ndogo na nyingine anaweka kwenye waleti, mwambie kila kitu lakini la kupekua si zuri kabisa, ipo siku utakuta hata vitu visivyokuhusu.

Kama ninavyokusema wewe mwanamke mwenzangu pia wapo wanaume wanaopekua pochi za wake zao hili nalo si sahihi kabisa, uaminifu uanzie kwenye penzi mpaka kila kitu kwani mnaweza kujikuta mnagombana kwa sababu ya kitu kidogo tu.

Leave A Reply