The House of Favourite Newspapers

Kwa Simba Hii… Kuna Swali?

0

WAWAKILISHI wa Tanzania, Simba jana walianza kwa kasi kwenye mchezo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa hatua ya kwanza kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Jwaneng Galaxy uliochezwa Uwanja wa Taifa wa Botswana.

 

Mabao yote mawili yalipachikwa ndani ya dakika 10 za mwanzo ambapo mtupiaji alikuwa ni nahodha John Bocco dakika ya pili baada ya kipa wa Jwaneng Ezekiel Morake kutema mpira wa kona iliyopigwa na Rally Bwalya ukakutana na mguu wa Bocco aliyeuzamisha wavuni pia ilionekana kiungo Taddeo Lwanga aliugusa mpira huo.

 

Dakika tatu mbele Bocco tena aliweza kuzamisha kambani waya wa pili baada ya mabeki kufanya makosa ndani ya 18 ilikuwa ni dakika ya tano tu ya mchezo.

 

Akiwa kwenye benchi la ufundi, Hitimana Thiery aliweza kushuhidia vijana wake wakikamilisha dakika 45 za kipindi cha kwanza wakiwa mbele kwa mabao mawili ambayo yaliweza kudumu mpaka mwisho wa mchezo huo.

 

Kocha Mkuu, Didier Gomes alikuwa jukwaani akishuhudia mchezo huo kwa kuwa hajakidhi vigezo vya Caf vinavyotaka makocha waweze kukaa kwenye benchi katika mechi za kimataifa lakini muda mwingi alionekana akiwa na mzuka haswa.

 

Shukrani kwa Aishi Manula kwa kuwa aliweza kuokoa hatari zilizofanywa na nyota wa Jwaneng dakika ya 20 baada ya mabeki wa Simba kushindwa kumzuia mshambuliaji wa wapinzani ambaye aliruka juu na kuupata mpira na kufanya jaribio kwa kichwa.

 

Pia Moagi Sechele naye alikuwa mwiba kwa Manula kwa kuwa alifanya jaribio dakika ya 37 liliweza kuokolewa na kipa huyu wa Taifa Stars.

 

Ilibaki kidogo Bwalya ambaye alikuwa mhimili eneo la kati kuweza kupachika bao la pigo la kona ilikuwa dakika ya 45 baada ya kona yake kuweza kuokolewa na kipa na kufanya lango la wapinzani hao kuwa salama.

 

YANGA YAIBUKIA BOTSWANA

Licha ya upinzani walionao ndani ya uwanja ila nje ya uwanja wamekuwa washkaji ndivyo ilivyokuwa jana ambapo wakati Simba ikiwa kwenye majukumu ya kitaifa jezi ya Yanga ilikuwa ndani ya uwanja wa taifa wa Botswana kushuhudia mchezo huo baada ya shabiki mmoja kuonekana akiwa ameivaa.

Leave A Reply