The House of Favourite Newspapers

Licha ya Kupiga Hat Trick, Tambwe Anyimwa Mpira Championiship

0

MSHAMBULIAJI wa DTB inayoshiriki Championship, Mrundi, Amissi Tambwe ameanza na rekodi ya kufunga mabao manne katika mchezo wa kwanza wa ligi hiyo dhidi ya African Lyon, lakini kilichowashangaza wengi ni kwamba hakuweza kupewa mpira wake wa hat trick.

 

Katika mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Tambwe alifunga mabao mawili katika kipindi cha kwanza na mabao mawili kipindi cha pili na kupelekea timu yake kuibuka na ushindi wa bao 4-1, katika mchezo huo.

 

Championi ambalo lilikuwepo kwenye mchezo huo lilimshuhudia mshambuliaji huyo ambaye ni nahodha wa timu hiyo akitoka bila ya kupewa mpira wake kama ilivyokuwa ikitarajiwa.

 

Baada ya mchezo huo, Championi Jumatatu lilimtafuta Ofisa habari wa Bodi ya Ligi, Karim Boimanda, ambaye alisema kuwa kawaida mchezaji aliyefunga ‘hat trick’ anatakiwa kupewa mpira kuanzia katika ligi ya daraja pili, Championship na ligi kuu.

 

“Sijui kwa nini hakupewa na sijajua kwa waliosimamia mchezo huo lakini kawaida mtu anatakiwa apewe mpira wake kama atakuwa amefunga ‘hat trick’ kuanzia daraja la pili, Championship na Ligi Kuu Bara,” alisema Boimanda.

 

Kwa upande wa Tambwe, alisema kuwa kwa sasa anachokiangalia ni kuisaidia timu yake kwa kuhakikisha inapata matokeo ya kila mchezo na hajui kwa nini hakupewa mpira wake.

IBRAHIM MUSSA, Dar es Salaam

Leave A Reply