Kamanda Mkondya: Uchaguzi 2020, Hatutapendelea chama chochote – Video
JESHI la Polisi nchini limesema limejipanga kuhakikisha Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu, utafanyika kwa haki na amani.
Pia limeahidi kuimarisha ulinzi na usalama katika kipindi chote cha uchaguzi huo bila kupendelea chama chochote cha siasa nchini.
Hayo yamesemwa leo Jumatano, Januari 8, 2020 na Mkuu wa Utawala wa Jeshi la Polisi nchini, DCP Lukas Mkondya katika mahojiano maalumu na Radio namba moja ya mtandaoni nchini, +255 Global Radio, alipotembelea ofisi za Makampuni ya Global Group zilizopo Sinza Mori, Dar.
DCP Mkondya ambaye aliambatana na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar, SACP Lazaro Mambosasa, alimwakilisha IGP Simon Sirro.
Katika ziara hiyo, Makamanda hao walitembelea vitengo mbalimbali vya makampuni ya Global Group kuanzia idara ya uzalishaji wa Magazeti Pendwa; Uwazi, Amani, Ijumaa, Ijumaa Wikienda, Risasi Mchanganyiko, Risasi na Jumamosi, Global TV Online na Global Digital.
“Jeshi la Polisi hatupendelei CCM wala chama chochote kingine cha siasa, kazi yetu ni kusimamia ulinzi na usalama wa raia na mali zao, tunahakikisha sheria za nchi zinatekelezwa na kusimamiwa bila upendeleo. Ukifanya uhalifu tutakushughulikia bila kujali chama chako cha siasa.
“Tunafahamu mwaka huu tunakabiliwa na uchaguzi mkuu, tumejipanga vizuri, wananchi msiwe na hofu, kila mtu akatekeleze haki yake ya kidemokrasia ya kuchagua kiongozi anayemtaka, kila mtu azingatie hali ya amani na utulivu. Uhuru bila sheria ni uendawazimu, tufuate sheria kwa utaratibu, ukifanya kazi nje ya hapo lazima tutakushughulikia.
“Tunapenda kutoa shukrani sana kwa wananchi wamekuwa wakishirikiana sana na jeshi la polisi kufichua mambo mbalimbali ya uhalifu. Polisi pekee hawawezi kufika kila sehemu, lakini wananchi wanafahamu maovu mengi yanayofanyika huko na wamekuwa wakitupatia taarifa na sisi tunazifanyia kazi na kuwakamata wahusika kisha kuwafikisha kwenye vyombo husika ili sheria ichukue mkondo wake.
“Changamoto kubwa iliyopo kwa sasa ni makosa ya ubakaji, mauaji, kujichukulia sheria mkononi. Sisi kama Jeshi la Polisi tumejipanga kutoa elimu kwa wananchi.. haya mambo wayakatae, wamrudie Mungu kwa dini zao ili waachane na haya mambo maovu kwa sababu ni kinyume cha sheria,” amesema Kamanda Mkondya.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL