The House of Favourite Newspapers

Mahakama Kuu Yatoa Maamuzi RUFAA YA MBOWE – Video

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam imesitisha kusikiliza rufaa ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe na Mbunge Esther Matiko, hadi hapo rufaa ya upande wa mashtaka ya kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kusikiliza rufaa ya viongozi wa CHADEMA, itakaposikilizwa katika Mahakama ya Rufani.

 

Uamuzi huo umetolewa mahakamani hapo leo kufuatia upande wa Serikali kukata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kukubali kusikiliza rufaa ya dhamana ya Mbowe na Matiko.

Awali, Jaji Sam Rumanyika wa Mahakama Kuu alitupilia mbali pingamizi la Serikali la kuzuia rufaa ya dhamana iliyokatwa na Mbowe na Matiko isisikilizwe na kuamua rufaa hiyo isikilizwe leo kuanzia saa 8 mchana.

 

Lakini Upande wa Serikali walikata rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kukubali kusikiliza rufaa ya dhamana ya Mbowe na Matiko, baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Jaji Sam Rumanyika aliahairisha kesi kwa nusu saa ili kuja kutoa uamuzi kama Mahakama Kuu iendelee kusikiliza rufaa hiyo au kusubiri uamuzi wa mahakama ya rufani.

 

Baada ya kurudi kutoa uamuzi huo, Jaji rumanyika ameamua Mahakama Kuu ya Tanzania isitishe kusikiliza rufaa hiyo hadi rufaa ya upande wa mashtaka ya kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kusikiliza rufaa hiyo itakaposikilizwa katika Mahakama ya Rufani.

 

Kwa mwenendo huo, suala hilo sasa limehamia kwenye mahakama ya Rufaa huku Mbowe na Matiko wakirudisha mahabusu ya Segerea mpaka rufaa itakapokamilika.

Mbowe na Matiko walifutiwa dhamana na Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, anayesikiliza kesi hiyo Novemba 23, mwaka huu kutokana na maombi ya upande wa mashtaka yaliyodai wameshindwa kuhudhuria mahakamani wakati kesi yao ilipopangwa kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali bila sababu za msingi.

 

Viongozi hao pamoja na wenzao saba wanakabiliwa na tuhuma za uchochezi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.

TAZAMA TUKIO HILO HAPA

Comments are closed.