Simba Yatangaza Kocha Mpya, Mfaransa Kutoka El Merrick (Picha +Video)
UONGOZI wa klabu ya Simba leo Januari 24, 2021 umemtambulisha rasmi Mfaransa, Didier Gomes Da Rosa kuwa Kocha Mkuu wa kikosi hicho mara baada ya aliyekuwa kocha wa kikosi hicho Sven Vandenbroeck kuachia ngazi Januari 7, mwaka huu.
Akimtambulisha mbele ya Waandishi wa Habari, Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez amesema kocha huyo amejiunga nao akitokea Sudan na amesaini mkataba wa miaka miwili.
“Tunamtambulisha kocha Gomes ametokea Al Merrikh ya Sudan na ni raia wa Ufaransa,” amesema Barbara
Tayari Simba ishamleta kocha wa makipa juzi na ameanza mazoezi na klabu hiyo jana kuelekea mashindano ya Simba Super Cup yatakayoanza Januari 27-31 na kuzikaribisha timu ya TP Mazembe ya DR Congo na Al Hilal ya Sudan.
Gomes ametokea Al Merrikh ya Sudan inayoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika ikiwa kundi moja na Simba.
Gomes ameshukuru kujiunga na Simba yenye malengo na ushawishi mkubwa kwa mashabiki.
“Nina furaha sana kuwa hapa na tuna nafasi ya kufanya mengi pamoja mbeleni. Timu niliyoondoka niliamua mwenyewe. Nataka kuwepo Simba kwa muda mrefu.”amesema Gomes