The House of Favourite Newspapers

Live Updates: Hatma Ya Rais Robert Mugabe Bado Haijulikani Zimbabwe

0
Rais Robert Mugabe.

Rais Robert Mugabe bado yuko katika kuzuizi cha nyumbani na hatma yake haijulikani. Alipo mke wake Grace, ambaye alikuwa na nia ya kumrithi kama rais na kuchangia hali iliyopo sasa hapajulikani.Baadhi ya ripoti zinasema kuwa amekimbia kwenda Namibia. Baadhi ya wanajeshi wako kwenye mitaa ya mji mkuu Harare na gari hili la wanajeshi hapo chini lilipigwa picha nje ya majengo ya bunge mapema leo.

Padri wa kanisa Katoliki, Kasisi.

Kasisi anayefanikisha mazungumzo Zimbabwe

Padri wa kanisa Katoliki ambaye ana urafiki wa karibu na familia ya Mugabe anahusika katika mazungumzo kati ya Rais Robert Mugabe na jeshi nchini humo – duru nchini humo zinasema – kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters.

Kasisi Fidelis Mukonori amekuwa rafiki wa rais huyo tangu miaka ya 1970, kwa mujibu wa makala kwenye gazeti la serikali la Herald iliyochapishwa miaka michache iliyopita.  Anachukuliwa kama “kiongozi wa kiroho” wa Mugabe.

 

Waziri akamatwa akitorokea Afrika Kusini

Mbunge ambaye pia ni waziri wa serikali Paul Chimedza, amekamatwa katika kizuizi cha barabarani akijaribu kukimbia kwenda Afrika Kusini, gazeti moja linasema nchini Zimbabwe. Gazeti hilo linasema kwamba alikamatwa eneo la Bubi kusini mwa nchi hiyo.

Mtu huyo ni waziri katika mkoa wa Masvingo na alikuwa  daktari kabla ya kujiunga na siasa.  Maafisa kadha wa Zanu-PF wanaripotiwa kuwa kizuizini akiwemo aliyekuwa mshirika mkuu wa Rais Robert Mugabe, Jonathan Moyo, na waziri wa fedha, Ignatius Chombo.

Mwanasiasa wa upinzani Tendai Biti.

Tendai Biti ataka kuwe na serikali ya mpito

Mwanasiasa wa upinzani Tendai Biti, ambaye alihudumu kama waziri wa fedha wakati wa serikali ya umoja nchini Zimbabwe kuanzia mwaka 2009 hadi 2013, anasema kuwa nchi inahitaji kwa dharura utawala wa mpito ili iweze kuendelea kidemokrasia.

Aliiambia BBC kuwa ana matumaini kuwa sasa mazungumzo yanaweza kuanza kati ya jeshi, watu wa Zimbabwe na wapatanishi wa eneo hilo.

Kiongozi huyo wa People’s Democratic Party, alisema kuwa hatua kijeshi zimeipata Zimbabwe kwa ghafla akisema kuwa hakufikiria kuwa Rais Mugabe anaweza kupitia hayo.

Mkuu wa UN ahimiza utulivu Zimbabwe

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ameomba kuwe na utulivu na kuvumiliana nchini Zimbabwe.

Msemaji wake, Farhan Haq, samesema Guterres anafuatilia kwa karibu yanayojiri Zimbabwe.

Ameongeza kuwa: “Kulindwa kwa haki za kimsingi, zikiwemo uhuru wa kujieleza na kutangamana, ni muhimu sana.”

Kwa mujibu wa shirika la AFP, Bw Guterres pia amesema jumuiya ya nchi za kusini mwa Afrika, SADC, inafanya juhudi kutanzua mzozo huo.

Namibia yakanusha Grace Mugabe kuwa huko

Naibu Waziri Mkuu nchini Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah, amekana uvumi kuwa nchi yake kuwa inamhifadhi  Grace Mugabe.

“Sijapokea taarifa kama hiyo. Kile ambacho tumejulishwa ni kuwa mke wa rais na familia yake wako salama nchini mwao,” alisema Nandi-Ndaitwah.

Bi Nandi-Ndaitwah ambaye pia anahudumu kama waziri wa mashauri ya nchi za kigeni, alinukuliwa akisema kuwa yale yanayoendelea katika taifa jirani  la Zimbabwe yanaleta wasiwasi mkubwa.

Raia wa Zimbabwe wanaoishi uhamishoni London wakiwa nje ya ubalozi wa taifa hilo nchini Uingereza.

Raia wa Zimbabwe nchini Uingereza washerehekea

Raia wa Zimbabwe wanaoishi uhamishoni London walikusanyika nje ya ubalozi wa taifa hilo nchini Uingereza, kusherehekea kinachoonekana kuwa kusambaratika kwa utawala wa Mugabe.

Wengi ni wanachama wa shirika ambalo limekuwa likiandaa maandamano mara kwa mara dhidi ya serikali ya Mugabe.

“Leo si kituo bali ni kikomo. Tunahitaji mabadiliko kamili,” alisema Chipo Parirenyatwa, mwenyekiti wa Shirika la Haki za Kibinadamu la Zimbabwe.

“Sifahamu ni vipi jeshi litaendesha mambo, lakini nina matumaini. Kuna haja ya kuwepo kwa uchaguzi kwa njia ya amani na jamii ya kimataifa kushirikishwa.

“Nafikiri kuna uwezekano wa 50-50 kwamba hilo litatokea.”

CHANZO; BBC SWAHILI

 

Leave A Reply