KAMPENI ya Uzalendo Kwanza iliyoanzishwa na Wasanii wa Filamu, Bongo Movie imezidi kuota mizizi baada ya kutanua matawi yake kwa mikoa yote ya Tanzania huku ikipata wanachama ambao ni wachezaji wa soka, wasanii wa muziki, wanasiasa na raia wa kawaida hapa nchini.
Akizungumza na wanahabari wakayi akiwapokea wanachama wapya, Mwenyekiti wa Chama hicho, Steve Mengele ‘Steve Nyerere’ amesema kuwa lengo la Chama hicho ni kuwafikia Watanzania wote kufahamu umhimu wa uzalendo, kuipenda nchi ikiwa ni pamoja na kushirikiana kikamilifu na serikali ya Rais John Magufuli katika kutimiza majukumu yake.
“Taifa la wazalendo linaanzia darasani, tunawaomba walimu wote wawe wazalendo kufundisha darasani, manesi na madakatari wawe wazalendo kutoa huduma zao, uzalendo pia ni mhimu kusapoti vilabu vyetu vya soka na Timu ya Taifa,” alisema Nyerere.
Aidha Nyerere amewaasa wanachama hao na Watanzania wote kuunganisha nguvu ya pamoja ili kulinda kazi zao za sanaa sambamba na kuwafanya Watanzania kupenda vilvivyo vyao mfano; kazi za wasanii wa ndani ili kukuza kipato chao na kuinua uchumi wa nchi.
Wacheza soka ambao wamejiunga na Uzalendo Kwanza ni; Mwanamtwa, Monja Liseki, Abdallah Kaburu, Dotto Mokili, Steven Nemes na wengine.
Mbali na hao, msanii wa Bongo Fleva, Ruby pia amejiunga na Uzalendo Kwanz ambaye amepewa jukumu la kutunga nyimbo za Uzalendo na video zake ili kufikisha ujumbe kwa wananchi wote.