Liverpool Yaipa Man United Kipigo cha Mbwa Koko
TIMU ya Manchester United wamepokea kichapo cha kihistoria baada ya kupigwa mabao matano kwa bila na mahasidi wao Liverpool katika dimba la Old Trafford. Mechi hiyo kali ya Ligi Kuu Uingereza, Mohamed Salah amefunga mabao matatu na kutoa assist moja, kazi ambayo ilizamisha kabisa jahazi la United.
Mashetani Wekundu waliingia katika mechi hiyo wakijivunia ushindi wa 3-2 dhidi ya Atalanta katika mechi ya Ligi ya Mabingwa mapema wiki hii. Hata hivyo, vijana wa Ole Gunnar Solskjaer walishindwa kuendeleza ubabe huo na kuongeza masaibu yao katika mechi hiyo ya nyumbani.
Wageni walitawala maeneo yote uwanjani huku Naby Keita akifungua ukurasa wa mabao katika dakika ya tano ya mchezo baada ya Bruno Fernandes kupoteza nafasi nzuri ya kufunga bao. Diogo Jota aliongeza bao la pili dakika nane kutokana na uzembe wa mabeki Luke Shaw na Harry Maguire.
Mason Greenwood alikaribia kufungia United katika dakika ya mwisho kuingia muda wa mapumziko kabla ya Salah kufanya mambo kuwa 3-0 akimalizia vyema krosi. Mzawa huyo wa Misri alifunga bao lake la pili katika dakika za nyongeza kabla ya kwenda mapumziko kabla ya kumalizia hat-trick yake dakika ya 50.
Dakika ya 50 Cristiano Ronaldo aliifungia Man U bao lakini lilikataliwa na mfumo wa usaidizi wa refa (VAR). Mambo yalikwenda mrama kwa United kunako dakika ya 60 baada ya Paul Pogba, ambaye aliingia kama mchezaji wa akiba kuliswa kadi nyekundu kwa kumchezea rafu Keita.
Ushindihuo umewafanya kupaa mpaka nafasi ya pili ya msimamo wa Ligi wakiwapiku Man City huku United wakishuka hadi nafasi ya saba.