UNAAMBIWA baada ya jana Kocha Mkuu wa Simba, raia wa Ufaransa, Didier Gomes Da Rosa, kumaliza mchezo wake wa kwanza dhidi ya AS Vita, amemgeuzia kibao straika wake mpya raia wa Nigeria, Junior Lokosa kwa kumtaka ahakikishe anakuwa fiti kabla ya mchezo wa marudiano na timu hiyo.
Simba jana usiku ilitarajiwa kumenyana na AS Vita kati mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho huko mjini Kinshasa DR Congo.
Simba imemsajili Lokosa ambaye hakusafiri na timu kwenda DR Congo, kwenye dirisha dogo msimu huu na amesaini mkataba wa miezi sita kwa ajili ya michuano ya kimataifa pekee, mshambuliaji huyu ni mzoefu kwani amewahi kucheza klabu kubwa kama Esperance ya Tunisia na Kano Pillars nchini kwao.
Sasa chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Simba kimeliambia Championi Jumamosikwamba, Kocha Da Rosa amemtaka Lokosa kuhakikisha anakuwa fiti kabla ya mchezo wa marudiano na AS Vita ili aingie katika kikosi kinachoshiriki michuano hiyo ya kimataifa ikiwa sambamba na kuongeza uzoefu wake kwa wenzake.
“Kocha amekuwa akilalamikia uzito na utimamu wa mwili wa Lokosa jambo ambalo lilimlazimu kutosafiri naye huku akimuachia majukumu mazito ya kufanya ili kikosi kitakaporejea awe ameonyesha kuwa tayari kwenye michezo ijayo.“
Pamoja na kutokuwepo nchini, kocha ameendelea kuulizia program alizomuachia Lokosa jambo ambalo ni wazi kwamba anahitaji kumtumia katika mchezo ujao sambamba na wengine aliokuwa amewaachia program,” kilisema chanzo hicho.
Alipotafutwa Meneja na Mratibu wa Simba, Abass Ally kuzungumzia ishu hiyo alisema: “Kuna wachezaji wengine walibaki sio Lokosa tu na waliachiwa program maalum ya kuhakikisha wanaifanya ili timu itakaporudi kutoka DR Congo basi waungane kwa ajili ya mechi zinazokuja.”
Stori na Musa Mateja, Dar es Salaam