The House of Favourite Newspapers

Lowassa Ammwagia Sifa Rais Magufuli

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa,  amepongeza utendaji kazi wa Rais John Magufuli ambapo amesema kampeni ya kutumbua watu ambao ni wazembe imesaidia nchi kushika adabu na mambo yanakwenda vizuri. 
Lowassa ameyasema hayo jana  katika mahafali ya Shule ya Msingi ya Meyers mjini Arusha.
“Rais  Magufuli anastahili pongezi, anafanya kazi nzuri sana, tunaona mawaziri wanafanya kazi nzuri, Waziri Mkuu (Kassim Majaliwa) yupo kule wengine huku, nchi imewaka moto kila sehemu,” amesema. Lowassa
Kwa mujibu wa Lowassa, kazi za Rais Magufuli, zinatakiwa kupakwa ‘poda’ kwa kuhusisha uboreshaji wa elimu ambayo itawapa ujuzi wahitimu kujiajiri.
“Kuna vijana wengi wanamaliza masomo kutokana na mpango wa elimu bure, sasa tujitahidi elimu hii iwasaidie vijana kupata ujuzi na ubunifu ili kuweza kujiajiri,”ameongeza.
Lowassa aliyejiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Julai 28, 2015,  na kupitishwa kuwa mgombea urais wa chama hicho akiungwa mkono na vyama rafiki vya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) alishindwa kuhimili mikikimikiki ya upinzani na kuamua kurejea ndani ya chama tawala, Chama Cha Mapinduzi  (CCM) Machi 1, mwaka huu.

Comments are closed.