Lwandamina Aanika Mikakati ya Usajili Azam
KOCHA Mkuu wa Azam FC, George Lwandamina amesema kuwa katika kuhakikisha mipango ya kutwaa ubingwa kwa timu hiyo inatimia, atakaa na uongozi wa timu hiyo ili kujua mchezaji wa kumsajili kwenye dirisha dogo.
Lwandamina ambaye alijiunga na Azam hivi karibuni akichukua mikoba ya aliyekuwa kocha mkuu wa timu hiyo, Aristica Cioaba, tayari amekaa kwenye benchi katika mechi moja dhidi ya Namungo ambayo iliisha sare ya mabao 2-2.
Azam FC kwa sasa inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa imevuna pointi 28 baada ya kucheza mechi 15, jana ilitarajiwa kucheza na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Chamazi.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Lwandamina alisema: “Hakuna kitu chochote ambacho nitaahidi kwa sasa kuhusu usajili lakini nitakaa na mkurugenzi kwa ajili ya kujua ni kitu gani nitakifanya kwenye kipindi hiki cha usajili.“
Kila siku kuna ushindani mkubwa ambao pia unachangia ligi kuwa ngumu na bora, na ligi ya Tanzania kwa sasa imezidi kuwa kubwa kwani watu wanafikiwa na taarifa popote walipo tofauti na zamani.”
Na Leen Essau, Dares Salaam