The House of Favourite Newspapers

MAAJABU YA KIFAA CHA TIBA MPYA YA UKIMWI

JANGA la ugonjwa wa Ukimwi lililodumu kwa zaidi ya miaka 36 linaweza kufikia kikomo endapo tiba mpya iliyogundulika nchi Marekani itakubaliwa na Shirika la Afya Duniani ‘WHO’. 

Weka kado tiba na majaribio yote ya kinga dhidi ya ugonjwa huo ulioua mabilioni ya watu, ugunduzi mpya uliofanywa na watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba cha Temple nchini Marekani ni kiboko kuliko zote.

 

Mmoja kati ya watafiti kutoka chuo hicho, Dk Kamel Khalili alijitokeza mbele ya wanahabari mjini Philadelphia na kusema:

 

“Ulimwengu unapaswa kufurahi pamoja nasi juu ya ugunduzi wenye mafanikio makubwa juu ya tiba ya ugonjwa wa Ukimwi tulioufanya.” Kizungumkuti kilichowakumba wanasayansi na watafiti wengi ni kushindwa kutenganisha Virusi Vya Ukimwi ‘VVU’ na vinasaba ‘DNA’ ndani ya mwili wa binadamu.

MAAJABU YA CRISPR

Dk. Khalili alisema ugunduzi wao umejikita zaidi kwenye kifaa walichokipa jina na CRISPR ambacho kina maajabu ya kuweza kuingia kwenye mfumo wa damu ya na kuvitoa virusi vya Ukimwi kutoka kwenye kinga ya mwili CD4 kisha kuviua kirahisi sana.

 

Majaribio mengi yaliyofanywa na watafiti yalishindwa kufikia hatua hii kwani tiba nyingi zilizokuwa zikitolewa kwa wagojwa zilikuwa zinaua VVU pamoja na seli za binadamu, jambo ambalo haliwezi kumsaidia mgojwa. Lakini Dk. Khalili anasema ugunduzi wao umezingatia hali ya mgonjwa kwamba anaweza kutolewa virusi vya Ukimwi, vikauawa na kuziacha seli zake katika hali nzuri kiafya.

 

Muda mfupi tangu ugunduzi wa watafiti hao kutoka Marekani utangazwe, taasisi nyingi za utafiti pamoja na madaktari kote ulimweguni wamekuwa wakipongeza hatua hiyo na kusema kuwa ni mwanga mpya wa kufikia kilele cha mafanikio ya kupata tiba ya Ukimwi.

 

Kama hilo halitoshi, katika taarifa yao Dk. Khalili na wenzake ambao uchunguzi wao waliufanya kupitia panya inasema kwamba, tiba yao haikuwalenga wagonjwa tu bali itazingatia pia kuwakinga wale ambao hawajaugua.

 

“Dawa yetu inakivuta kirusi nje ya seli (CD4) bila kuiathiri seli yenyewe na kukiua. “Hivyo, dawa hii itatumika kwa muda fulani na kuua virusi vyote mwilini na hakuna haja ya kuitumia wakati wote kama ilivyo dawa ya kufubaza VVU (ARV),” alisema Dk. Khalili.

 

Habari hii imepokelewa kwa mtazamo chanya na mmoja wa wataalamu katika Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu Kituo cha Mbeya (NIMR-MMRC), Clifford Majani ambaye alisema utafiti huo ni mwanga mpya katika teknolojia ya kukabili VVU.

“Kama imepatikana teknolojia ya kukiondoa kirusi ndani ya seli ni hatua nzuri ya kukabili VVU. Jambo hili lilionekana kuwa gumu mwanzoni,” alisema Majani. Mara kadhaa wanasayansi wamekuwa wakitengeneza tiba za VVU kwa kutengeneza dawa itakayoweza kutambua seli zilizoathirika ili ziuawe lakini hilo limekuwa gumu kuleta matokeo.

 

Hata hivyo, wasiwasi ambao baadhi wa madaktari wameuonesha kwenye tiba hiyo mpya ni uwepo wa usalama kwa mtu atakayetibiwa, jambo ambalo wagunduzi hao katika taarifa yao wamesema wamezingatia kwa kiwango cha juu.

 

Muda ambao umewekwa na wagunduzi hao ni miaka michache ijayo ili tiba yao ianze kutumika kote duniani na kwamba wanasubiri ruhusa ya WHO. Ugunduzi huu wa tiba mpya umekuja wakati ambapo kumekuwa na vuguvugu kutoka kwa baadhi ya wagunduzi wa tiba ya Ukimwi wakionesha hali ya kuanza kukata tamaa kupata tiba ya Ukimwi.

 

Katika mkutano wao wa hivi karibuni uliofanyika Melbourne, Australia wanasayansi kadhaa wanaotoka kwenye taasisi kubwa za utafiti za VVU wameweka wazi kuwa tafiti nyingi zilizokuwa na matumaini zimeshindwa kufanya kazi kwa asilimia 100.

 

Walisema, pamoja na dawa nyingi duniani kufanyiwa majaribio na kuonesha uwezo wa kutibu Ukimwi hali hiyo imekuwa ikifanyika kwa muda mfupi tu kwa mgonjwa kwani baada ya kutumia dawa na kuonekana amepona virusi huchipuka upya.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti ya wa Magonjwa ya Kuambukiza na Kinga ya Peter Doherty ya Australia, Profesa Sharon Lewin alionesha wasiwasi wake juu ya dawa mpya zinazoendelea kugunduliwa. Hata hivyo, Dk Khalili alisema wametengeneza dawa yao kwa protini maalumu ambayo inakata sehemu ya seli iliyoshambuliwa na kirusi cha Ukimwi na kukivuta nje.

 

Baada ya kukivuta, dawa huachana na seli hiyo na kuiacha ikijitibu yenyewe na kupona kabisa kiasi cha kuendelea na kazi zake za kinga mwilini mwa binadamu bila tatizo. VVU kwa kawaida hushambulia seli kinga aina ya CD4 na kuzifanya kama kiwanda cha kuzalishia virusi vingine hatari katika mwili wa binadamu.

 

Ugunduzi wa Dk. Khalili na wenzake uliandikwa katika Jarida la Taifa la Elimu ya Sayansi la National Academy of Science la Marekani na kuonekana kuvuta hisia za wengi. Hata hivyo, serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Afya inayoongozwa na Waziri Ummy Mwalimu imekuwa ikieleza kuwa, bado tiba ya Ukimwi haijapatikana na kuwataka wananchi kuchukua tahari ya kujikinga na ugonjwa huo hatari.

Richard Manyota  na mitandao

MAJERUHI WA AZAM HOI KITANDANI AZUNGUMZA – VIDEO

Comments are closed.