The House of Favourite Newspapers

Mabilionea wasio na huruma 43

0

American Dollars Wallpaper 1435ANACHOKIHITAJI Inspekta Masala ili aweze kuwatia mikononi mwake wauaji Dk Viola na Vanessa, ni picha zinazoonyesha sura zao baada ya upasuaji wa kubadilisha sura uliofanywa na Dk Jeremy Ho huko Bangkok, Thailand.

Anazihitaji picha hizo haraka, alishamwomba Dk Jeremy akakataa kumpa akidai ilikuwa ni siri yake na wateja wake, ameamua kwenda kujaribu tena kuziomba lakini alipofika kwenye hospitali hiyo akapewa taarifa za kusikitisha kuwa Dk Ho amefariki kifo kinachofanana na kile cha wapelelezi aliokuwa nao Inspekta Masala, hii inaonyesha kuwa muuaji ni mmoja na anafanya hivyo ili kuzuia ukweli kujulikana.

Akiwa hapo msibani, Inspekta Masala anakutana na kijana aliyebadilisha jinsia na kuwa mwanamke, huyo ni Jen ambaye amemwambia alipiga picha na Dk Viola na Vanessa kabla na baada ya upasuaji, yuko tayari kumpatia picha hizo kama tu atakubali kufanya naye ngono! Inspekta Masala ametafakari kwa muda na mwisho akatoa jibu moja tu; I AM READY! Akimaanisha yuko tayari.Je, nini kitaendelea?SONGA NAYO…

MOYONI mwake Inspekta Masala hakutaka kabisa kufanya kitendo hicho, hasa alipouangalia ukweli kwamba Jen hakuzaliwa mwanamke na tendo la ndoa kwa Inspekta Masala kwa alivyojifunza tangu utotoni lilikuwa ni kati ya mwanamke na mwanaume, tofauti na hapo ilikuwa ni dhambi.

“Ninafanyaje hapa wakati picha nazihitaji na sharti lake ni lazima nifanye ngono? Potelea mbali, mimi mtoto wa kiume niko kazini, maringo yote kando, Simba akizidiwa hula hata nyasi!” aliwaza Inspekta Masala akimwangalia Jen, katika maisha yake hakuwahi kuwaza kulikuwa na wanaume wenye sura nzuri kiasi hicho, haikuwa rahisi kabisa kugundua alizaliwa mwanaume.

Jen alikuwa akitabasamu huku akimwangalia Inspekta Masala kwa jicho la tamaa kuanzia kichwani kuelekea miguuni, mwili wake ulijengeka vizuri sababu ya mazoezi na alikuwa na urefu wa kutosha kumvutia mwanamke yeyote aliyemwangalia, kitu ambacho wanawake wengi hawakukipenda kabisa; kitambi hakikuwepo tumboni mwake.

“You have great body!”(Una mwili mzuri!)
“Thank you!”(Ahsante!)

“Are you sure you are ready to go?”(Una uhakika upo tayari kwenda?)
“Yes, I am sure, I need those photos like I everyday need oxygen to survive!”(Ndiyo, nina uhakika, ninazihitaji picha hizo kama ninavyohitaji hewa ya oksijeni kila siku ili niishi!)
Ni kweli wapelelezi wote aliokuwa nao Inspekta Masala walishakufa, yeye peke yake ndiye alikuwa amebaki na moyoni kulikuwa na hisia kwamba angekufa wakati wowote na huo ndiyo ungekuwa mwisho wa msako wa Dk Viola na nduguye Vanessa, upande fulani wa akili yake ulimwambia awe makini sana na mwanamke aliyekuwa akiongea naye kwani angeweza kuwa miongoni mwa waliotumwa ili kumwingiza mtegoni.

Hakumwonyesha Jen hisia hizo, mwisho wa maziko aliingia ndani ya nyumba ya Dk Jeremy Ho akiongozana na Jen kwenda kumwona mjane wa marehemu na kumpa pole, baada ya zoezi hilo hapakuwa na sababu nyingine tena ya kuwafanya waendelee kuwa maeneo hayo, wakakubaliana kuondoka, kila mtu ndani ya gari lake, Jen akiwa mbele na Inspekta Masala akimfuata kwa nyuma.

Walipita katikati ya Jiji la Bangkok na kuzidi kusonga mbele kuelekea maeneo ya Soi Tonson walikoishi matajiri wa jiji hilo na watu mbalimbali wenye majina makubwa, gari ya Jen ilisimama mbele ya jengo la ghorofa mbili, lango likafunguliwa na kuzama ndani, Inspekta Masala akafuata kwa nyuma na kuegesha kando yake.
“Unaishi hapa?”
“Ndiyo.”

“Umepanga?”
“Hapana, ni nyumba yangu!”
“Haiwezekani!”
“Kwa nini?”
“Ni ya kifahari mno.”

“Kwani mimi siyo wa kifahari?”
“Sawa lakini si kiasi cha kulingana na nyumba hii, unaishi hapa na nani?”
“Peke yangu na mbwa wangu tu.”
“Duh! Kweli umeyapatia.”

Wakazama ndani na kupandisha moja kwa moja hadi chumbani kwa Jen, ghorofa ya kwanza ambako walipoingia tu kitu cha kwanza alichokifanya Jen ni kuvua nguo zote na kubaki kama alivyozaliwa, Inspekta Masala akashangazwa na ukubwa wa matiti yake.
“Ni kweli ulizaliwa mwanaume?”
“Ndiyo.”

“Naweza kuona picha zako za zamani?”
“Haina shida, nitakuonyesha, ziko hapo kwenye droo ndani ya albamu iliyobeba picha zote zikiwemo pia unazozitafuta.”

“Ndiyo kilichonileta hapa, kuona hizo picha na niko tayari kufanya chochote ili nizione!”
“Nitakuonyesha, kaoge kwanza halafu utimize sharti nililokupa, baada ya hapo nikukabidhi picha.”
“Hakuna shida.”

Bila kupoteza wakati Inspekta Masala aliomba kuonyeshwa chumba cha bafu ambacho kilikuwa kando tu mwa kitanda, akaingia huko na nguo zake zote, hakutaka kuvua mbele ya Jen. Siku zote alikuwa ni mtu wa kuoga vizuri na kusugua kila sehemu lakini siku hiyo hali ilikuwa tofauti, alichofanya ni kujimwagia maji kama bata wafanyavyo ndani ya dimbwi, haukupita muda wa dakika kumi akawa ametokeza chumbani na kushangazwa na taswira aliyoikuta kitandani.

“Mungu wangu!” alipiga kelele baada ya kumwona Jen amelala chali kitandani, uso wake ukiwa umefumuliwa kwa risasi na damu nyingi kama dimbwi zikiwa zimezunguka kichwa chake.

Alipotupa macho dirishani, aliona kioo kikiwa kimevunjika, ishara kwamba risasi ilipitia hapo. Moyo ukaanza kumuenda mbio na jasho jingi kumtoka huku akijiuliza maswali mengi bila majibu, kubwa likiwa ni nani aliyempiga risasi Jen wakati ndani ya nyumba hiyo walikuwemo watu wawili tu? Hakupata jibu, wasiwasi ukazidi kumwingia, machozi ya uchungu yakamtoka kwa sababu Jen alikuwa amekufa kwa sababu yake kabla hata hajamkabidhi picha alizozifuata.

“Lazima nizitafute! Bila kuzipata hawa wauaji sitawakamata,” aliwaza Inspekta Masala na kuzivamia droo zote zilizokuwepo chumbani humo akizivuta na kumwaga kila kitu, macho yake yakitafuta albamu za picha, kwenye droo ya kitanda macho yake yaligongana na albamu mbili, zikiwa zimejaa picha na kuanza kuzipitia moja baada ya nyingine huku mwili ukitetemeka, maana maiti ya Jen ilikuwa bado imelala kando yake, lilikuwa ni jambo la kuogofya mno lakini alijipa moyo na kufanya kazi kwa ujasiri.

“Hureee! Hureee!” alishangilia baada ya kuona picha mbili ambazo Jen alipiga na watu wawili wakiwa na sura tofauti, kilichomfanya awatambue ni aina ya nguo walizovalia, zilikuwa ni zilezile katika picha ya kwanza na ya pili, tofauti ilikuwa ni sura, katika picha ya pili walionekana ni wazee wa Kijapan, ingawa mikono yao ilikuwa na rangi ya Kiafrika.

Hapakuwa na ubishi wowote wala wasiwasi kwamba taswira za watu aliokuwa akiwaangalia hawakuwa Dk Viola na nduguye Vanessa, asimilia mia mbili alikuwa na uhakika kwamba hao ndiyo watu aliokuwa akiwasaka kwa udi na uvumba, akageuka kando yake na kumwangalia Jen, roho ikamuuma, lakini akamshukuru kwa msaada aliompa na akaahidi kwamba damu yake iliyomwagika siku hiyo ndiyo ingekuwa chachu ya kuwakamata Dk Viola na Vanessa kuwafikisha mbele ya sheria.

“Inabidi nimpigie simu bosi wangu kumjulisha juu ya jambo hili!” aliwaza Inspekta Masala na kuingiza mkono mfukoni mwake ambako alichukua simu yake aina ya Samsung na kutafuta namba ya Mkurugenzi wa Scotland Yard.
“Niambie Inspekta!”

“Nimefanya kazi nzuri lakini imegharimu maisha ya mtu mmoja.”
“Nani tena?”
“Nilikutana na sijui nimwite kaka au dada ambaye alipiga picha na Dk Viola na Vanessa kabla na baada ya upasuaji!”
“Ulikutana naye wapi?”
“Kwenye msiba.”

“Wa nani?”
“Dk Jeremy Ho.”
“Taarifa zake ninazo, endelea!”
“Huyu msichana akakubali kuja nyumbani kwake kunipa hizo picha, tukiwa chumbani kwake nikamwacha kwenda kuoga, niliporejea nikakuta amepigwa risasi na kufa palepale!”

“Mungu wangu! Picha umepata?”
“Nimepekua mpaka nimezipata.”
“Kazi nzuri, unachotakiwa kufanya ni kuwapigia simu polisi, uwaeleze mahali ulipo na kilichotokea, usiwe na wasiwasi, kila kitu kimedhibitiwa na kuna watu wanafuatilia mambo unayoyafanya ili kuona kwamba uko salama!”

“Sawa mkuu, naondoka hapa sasa hivi baada ya kumpigia simu mkuu wa upelelezi wa hapa Bangkok.”

“Hakuna shida, mambo mengi fungua barua pepe yako nimekuandikia mpango mzima uliopo, maana unasakwa kwa udi na uvumba uuawe, kama usingekuwa bafuni, jamaa wangekuwa wamekuua!”

“Sawa, nitasoma sasa hivi,” Inspekta Masala aliitikia na kukata simu, kisha kuinamisha kichwa chake na kumbusu Jen shavuni.

Alichokifanya ni kushuka haraka sana hadi chini ambako aliangaza macho yake huku na kule, bastola ikiwa mkononi, alipohakikisha hakuna mtu yeyote, alikimbilia moja kwa moja kwenye gari lake na kuanza kurudi kinyumenyume kuelekea kwenye lango la kutokea, akasimama hapo bila kujua cha kufanya kwani lango hilo lilifunguliwa kwa rimoti ambayo hakuwa nayo.

Mara moja akachomoka ndani ya gari na kurejea tena hadi chumbani ambako alichukua lundo la funguo lililokuwa na rimoti na kuja nalo hadi garini, alipobonyeza lango likafunguka na kutoka bila matatizo yoyote akiendesha kwa kasi kama gari ya mashindano, mbele kidogo alipishana na magari ya polisi, huku akihema akaegesha kando ya barabara na kufungua kompyuta yake ili asome barua pepe aliyotumiwa na bosi wake, maelekezo yote yalikuwa humo.

Alipomaliza alizima kompyuta na kuanza kuendesha tena gari lake kwa kasi, lengo lake afike hotelini salama, kilometa kama moja hivi kabla hajaingia katikati ya jiji, alishangaa kuona magari mawili yamesimama katikati ya barabara yote yakiwa yamewasha taa zake kali, moyo wake ukashtuka na kuanza kwenda mbio, alichokifanya ni kuichomoa bastola yake kiunoni na kuishikilia, mbele ya magari hayo alisimama, taa zikazimwa, akamulikwa na tochi.

“Shuka!”
“Ninyi ni akina nani?”
“Usiulize maswali!”

Je, nini kitaendelea? Nini kitampata Inspekta Masala? Huu ndiyo mwisho wake? Fuatilia siku ya Ijumaa katika Gazeti la Championi Ijumaa.

Leave A Reply