The House of Favourite Newspapers

MADAI YA KUFUNGA NDOA, KUVAA PETE, KUNASA UJAUZITO, LULU AANIKA UKWELI WOTE

STAA wa filamu za Kibongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’, hivi karibuni alifungukia madai yote yaliyokuwa yakizungumzwa mitandaoni juu yake kuvua pete ya uchumba, kunasa ujauzito na kufunga ndoa alipokuwa nchini China, Risasi Jumamosi limenasa mazungumzo hayo.  

 

Akizungumza ukweli wa moyo wake kupitia Kipindi cha Play List cha mtangazaji Lily Ommy wa Radio Times FM, Lulu alieleza mambo hayo matatu ambayo yamekuwa yakizungumzwa mno kwenye mitandao ya kijamii. Mambo hayo yaliibuka kutokana na yeye kutozungumza na vyombo vya habari mara kwa mara ambapo alianza na lile la kuvua pete.

 

KUVUA PETE YA UCHUMBA

Akianza na lile la kuvua pete ya uchumba, Lulu alianika ukweli kuwa, kuna wakati watu huanzisha mambo yao ili wapate lile wanalolihitaji ingawa kwake yeye anaona kuvua pete ni jambo la kawaida kama mambo mengine kisha akatoa mfano wa kuvua pete na kuiweka mezani.

 

“Unajua haya mambo haya mimi nilishafanya sana, unaanzisha kitu ili upate kitu, sasa siwezi kuwazuia watu kusema juu ya hili,” alisema Lulu ambaye baadaye kabisa mwishoni wa mahojiano alikiri kuvua pete hiyo kwenye maswali ya NDIYO na HAPANA.

KUNASA UJAUZITO

Akizungumzia ishu ya yeye kunasa ujauzito alipotoka gerezani kutokana na jinsi alivyokuwa akionekana kuwa mnene, Lulu alisema kuwa haukuwa ujauzito kama watu walivyodhani, bali alinenepa mno kiasi cha watu kuhisi hivyo kutokana na unene wake kumfanya aonekane kama mjamzito.

 

“Unajua mimi nikinenepa ni asili ya mwili wangu, nina mguu mnene sana hivyo uliongezeka, mwili pia uliongezeka kwa kiasi kikubwa kwani niliongezeka kilo 20 hivyo kila mtu aliamini nina ujauzito, sikuwa na ujauzito,” alifafanua Lulu.

KUFUNGA NDOA

Alimalizia kwa kusema kuwa yeye hajafunga ndoa nchini China kama watu wanavyodai, bali alikwenda kwa ajili ya matembezi tu. “Mimi sijafunga ndoa China kama watu wanavyodai na watu wanaongea kwa sababu sina kawaida ya kutangaza mahusiano yangu.

 

Mimi naamini mahusiano yangu si maarufu, umaarufu ni wangu hivyo sioni haja ya kutangaza mambo yangu, hivi ndoa huwa inatangazwa jamani?” Alihoji Lulu ambaye alifunga mjadala kwa kusema kuwa kama ambavyo hakutangaza sherehe yake ya kuvishwa pete ya uchumba, hata ndoa yake si ya matangazo.

STORI: Mwandishi Wetu

 

JIUNGE NA FAMILIA YA GLOBAL TV UPANDE MTANDAO WA MAFANIKIO

Bofya hapa kujiunga na familia ya Global TV Club ==> Global TV Family Club

Comments are closed.