Madaktari 24 kutoka Hospital ya Asan Medical Centre, Korea Kusini, wamewasili jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kutoa huduma za bure za matibabu maeneo mbalimbali nchini Tanzania hususani mkoani Mwanza.
Taarifa iliyotolewa baada ya kuwasili kwa madaktari hao ilisema watakwenda Mwanza ambako watatoa matibabu katika Hospitali ya Sangabuye,Wilaya ya Ilemela mkoani humo kisha hospitali za Mwangika na Isole wilayani Sengerema.
Miongoni mwa waliojitokeza kuwapokea ni Diwani wa Kata ya Katunguru na Mwenyekiti Mstaafu wa Wilaya ya Sengerema, Mathew Lubongeja, Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Global Groups, Eric Shigongo, ambaye ni mdau.
Akizungumza na wanahabri, kiongozi wa madaktari hao alisema jopo hilo limejipanga vizuri kutoa huduma hiyo kwa wakazi wa Kanda ya Ziwa na Zanzibar na wengine watakaojitokeza ambapo watashirikiana na madaktari bingwa watatu wa nchini.
Aidha amesifia amani na utulivu nchini hapa akisema vitawafanya watekeleze wajibu wao huo kwa amani na ufanisi katika kuisaidia jamii katika masuala ya afya.
Naye mwenyeji wao, Mathew Lubongeja, ambaye pia ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Yonam nchini Korea Kusini amesema amewapongeza madaktari hao kurejea tena hapa nchini tangu walipokuja kwa mara ya kwanza mwaka 2016 walipotoa tiba kwa ufanisi mkubwa, jambo linaloonyesha wanavyoipenda Tanzania.
Kwa upande wake Shigongo aliwashukuru madaktari hao kwa ujio wao nchini akisema ni faraja kwa wakazi wa vijijini ambao watapatiwa huduma hizo.
“Nipo hapa kwa niaba ya wananchi wa Buchosa ambako mimi ninatokea, wawashukuru sana madaktari hawa kwa kujitoa kwao kuja hapa nchini hasa kwenda maeneo ya vijijini ambako kuna uhaba mkubwa wa madaktari na vifaa tiba.
“Nazishukuru serikali za Tanzania na Korea kwa kuwezesha jambo hili liweze kutokea, hii ni fursa kwa wakazi wa Sengerema, Mwangika, Buchosa na Isole kujitokeza kwa wingi kupatiwa tiba na madaktari hawa,” alisema Shigongo.
Comments are closed.