The House of Favourite Newspapers

Madhara Ya Kula Chipsi, Mayai, Kuku Na Soda!

LEO tutazungumzia vyakula hatari kwa afya zetu. Vyakula tunavyotakiwa kuvila, hatuvili na pengine upatikanaji wake ni wa shida, hivyo tunalazimika kula vilivyopo licha ya kuwa vina madhara kwa afya zetu.

Hali hii imeongeza idadi ya wagonjwa na magonjwa sugu. Chakula kikuu cha mijini ni chips, kuku, mayai, soda, juisi za makopo au paketi, nyama choma na pombe. Pia kuna mkate mweupe, maandazi na chapati. Vyakula hivi huliwa kila siku, lakini ukivichambua utagundua vina madhara makubwa kiafya kama tutakavyoona hapa chini.

CHIPS

Chips ambayo kwa kawaida hutengenezwa kutokana na viazi mviringo na kukaangwa kwenye mafuta, ni chakula kinachotakiwa kuliwa kwa kiasi kidogo sana na kwa nadra sana, kwa sababu kiko kwenye kundi la vyakula vyenye mafuta mengi ambavyo huliwa kwa uchache.

KUKU

Kwa kawaida, kuku wengi wanaotumika kwenye biashara ni kuku wa kisasa. Nyama ya kuku hawa haina virutubisho sawa na kuku wa kienyeji. Hii inatokana na ukweli kwamba kuku hao hulishwa madawa mbalimbali ya kuwakinga na magonjwa na hulishwa vyakula vilivyochanganywa madawa ili wakue haraka. Kwa mazingira hayo, nyama itokanayo na kuku wa aina hii haiwezi kuwa bora.

Kiasili kuku huishi mazingira huru kwa kula vyakula ambavyo hujenga na kuukinga mwili wake dhidi ya magonjwa mbalimbali, kuku wa aina hii ndiye anayefaa kuliwa na kuleta faida ya nyama ya kuku inayokusudiwa.

MAYAI

Halikadhalika, mayai yanayopatikana kwa wingi mijini ni yale yatokanayo na kuku wa kufuga wa kisasa. Kiasili, mayai ya kuku wa kufuga, hayawezi kuwa sawa na mayai yatokanayo na kuku wa kienyeji.

Huhitaji kuwa mwanasayansi kuona tofauti kati ya yai la kuku wa kienyeji na kuku wa kufuga, kwani mayai hayo yakipikwa huwa tofauti kwa ladha na hata rangi. Ni ukweli ulio wazi kuwa kuku wa kufugwa hulishwa vyakula vya kutengeneza ambavyo ndani yake huwekwa kemikali na madawa mbalimbali, wakati kuku wa kienyeji hula vyakula asili kwa kujitafutia wenyewe na mazingira wanayoishi ndiyo yanayowafanya wawe tofauti na bora. Hivyo ni dhahiri kwamba mayai tunayokula ya kuku wa kisasa yana madhara zaidi kuliko faida mwilini.

 

SODA

Moja ya vinywaji vinavyopendwa na kutumiwa na watu wengi ni soda. Wengi hudhani ni kinywaji ambacho hakina madhara kabisa kwa mtumiaji. Familia nyingi zimeamini kuwa soda ni kinywaji bora na hata watoto wetu wamerithishwa imani hii. Lakini kwa upande wa pili wa kinywaji hiki, siyo kinywaji salama kama ambavyo imekuwa ikielezwa. Siwezi kusema moja kwa moja kuwa mtu huruhusiwi kabisa kunywa soda lakini watu walitakiwa kuelimishwa na kuelezwa madhara ya kupenda kunywa soda na athari anazoweza kuzipata mtu kiafya. Naamini tahadhari inayotolewa kwa wanywa pombe na wavuta sigara ingefanywa pia kwa wanywa soda.

Utafiti unaonesha kuwa soda, huwekwa sukari nyingi kiasi kisichopungua vijiko sita katika chupa moja. Kiwango hicho cha sukari ni kingi zaidi ya mara tano ya kile kinachoruhusiwa kwa mtu kutumia kwa siku. Madhara ya sukari mwilini ni mengi, yakiwemo ya kudhoofisha kinga ya mwili na viungo kwenye sehemu za maungio na pia huongeza uzito wa mwili. Ukitaka kujua soda ina madhara kiafya, fanya utafiti binafsi na utagundua haya ninayoyaandika.

Kunywa soda zisizopungua tatu kwa muda mfupi, kisha lala usiku kama kawaida halafu wakati wa kuamka asubuhi, usikilize mwili wako. Utaamka ukiwa na maumivu mwili mzima, utajihisi uchovu, hasa sehemu za maungio, mfano wa mtu aliyefanya mazoezi mazito au kazi nzito siku iliyopita. Hiyo ni

kutokana na kuingiza kiwango kingi cha sukari mwilini.

JUISI

Wengi hudhani juisi ni kinywaji baridi kisicho na kilevi wala madhara kwa mnywaji. Lakini utakuwa sahihi ukizungumzia juisi zilizotengenezwa kwa matunda halisi bila kuongezewa vitu vingine. Siku hizi juisi nyingi zinazouzwa kila sehemu ni zile zilizoongezwa sukari nyingi.

Juisi nyingi hutengenezwa kwa kuchanganya maji, sukari na rangi zilizotengenezwa kwa kemikali mbalimbali zikiwemo zenye ladha ya matunda (siyo matunda halisi). Juisi za aina hii ndiyo nyingi na zinapatikana kila kona ya nchi hii, waathirika zaidi wakiwa watoto wetu ambao hupenda kunywa kwa kufuata utamu wa sukari nyingi zilizowekwa na ladha za matunda.

Utafiti umeonesha kemikali zinazowekwa kwenye vinywaji hivi vya kwenye makopo au plastiki, hudhoofisha kinga ya mwili na huwa chanzo cha magonjwa ya saratani na mengine hatarishi. Nakusihi kuacha kunywa kabisa juisi hizo na usimpe mwanao. Badala yake tengeneza juisi wenyewe kwa kutumia matunda halisi ili kupata faida katika miili yetu.

Comments are closed.