RAIS John Magufuli amemuagiza Waziri mpya wa Madini, Dotto Biteko, kuhakikisha anajenga vituo vya madini vitakavyosaidia kuratibu biashara ya madini hayo ili Serikali isipoteze mapato yake na wananchi waweze kunufaika.
Magufuli amesema hayo leo Jumatano, Januari 9, 2019 baada ya kuwaapisha viongozi mbalimbali aliowateua jana akiwemo waziri huyo na aliposlema sekta ya madini bado ina changamoto kubwa na kwamba nchi inayoongoza kwa Afrika Mashariki kwa kuuza dhahabu siyo Tanzania japo ndiyo mzalishaji mkubwa.
“Dhahabu yetu hailinufaishi taifa, Wizara ya Madini tumewahi kujiuliza madini yanayochimbwa yanaenda kuuzwa wapi? Najua kwenye sheria inatakiwa kuanzishwa kwa ‘mineral centres’ lakini tujiulize, zimeanzishwa ngapi? Ziko wapi? Inauma ukiona zaidi ya kilo 300 zinasafirishwa. Je, zimesafirishwa ngapi?
“Ndio maana nafukuza hata mawaziri siyo kama siwapendi, wengine ni marafiki zangu, lakini utafanya nini sasa lazima tufanye kazi. Mimi nitaendelea kufanya mabadiliko kila mahali, ambapo nitakuwa sijaridhika; anayehusika ataondoka, hata Biteko nimekuteua lakini nikiona haparidhishi utaondoka. Kama mtu hawajibiki anaondoka tu, Tume ya Madini ikafanye kazi, lazima tuanzishe vituo vya madini kila mahala ili udhibiti wa madini uwe wa hali ya juu.
Rais alimwagiza Biteko kuanzisha mfumo wa vituo hivyo huko Geita na maeneo mengine akimwelekeza kushirikiana na Wizara ya Fedha na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania ili kuanza kununua dhahabu nchini.
Aliyesema hayo kutokana na kutokuwepo kwa uratibu wa jinsi dhahabu hiyo inavyopatikana na mahali inapouzwa, ambapo sehemu kubwa huuzwa na kutoroshwa na wafanya magendo na kuifanya serikali kutojua mzunguko mzima wa dhahabu hiyo.
Alisisitiza kwamba pakiwepo mfumo thabiti wa kufuatilia uzalishaji na uuzaji wa dhahabu kwa kupitia vyombo vya serikali, madini hayo yanaweza kutumika kama njia ya kurudisha thamani ya shilingi nchini.
Comments are closed.