The House of Favourite Newspapers

MAHAKAMA YA TANZANIA KUWAJENGEA UWEZO MAHAKIMU WAPYA

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kulia) akimuapisha Bi. Mfanyeje Omari Banza kuwa Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, wanaoshuhudia wa pili kushoto ni Naibu Msajili Mwandamizi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Messeka Chaba, kushoto kwake ni Mtendaji anayeshughulikia Mahakama za Mwanzo nchini, Bw. Humphrey Paya.
Wakisaini hati za kiapo.
Mhe. Jaji Mkuu akimpongeza Mhe. Banza kwa kuwa Hakimu mara baada ya kumuapisha rasmi.
Pichani ni Mhe. Mfanyeje Omari Banza, Hakimu mpya aliyeapishwa na Mhe. Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Mhe. Banza mara baada ya kumuapisha, wa kwanza kushoto kwa Mhe. Jaji Mkuu ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi pamoja na baadhi ya Maafisa walioshiriki katika hafla fupi ya kuapishwa.

 

Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto imeandaa utaratibu wa kuwapatia mafunzo maalum Mahakimu wapya wanaoajiriwa yatakayowawezesha kutimiza wajibu wao kwa weledi.

 

 

Hayo yamezungumzwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma Aprili 25, 2019 Ofisini kwake Mahakama ya Rufani-Dar es Salaam mara baada ya kumuapisha rasmi Mhe. Mfanyeje Omari Banza, kuwa Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo.

 

 

“Tofauti na miaka ya nyuma, kuanzia mwaka huu Mahakimu wote watakaoajiriwa watahudhuria mafunzo maalumu yatakayokuwa yanaendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama  Lushoto ili kuwajengea uwezo utakaowawezesha kutimiza majukumu yao vyema” alieleza Mhe. Jaji Mkuu.

 

 

Kwa upande mwingine, Mhe. Jaji Mkuu amemuasa Mhe. Banza kutimiza majukumu yake ya utoaji haki kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizopo ikiwa ni pamoja na  kutojihusisha na vitendo vya rushwa.

 

 

“Mahakama tunatuhumiwa sana kwa kujihusisha na vitendo vya rushwa, hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kukemea vitendo hivyo ili kurejesha taswira nzuri ya Mahakama kwa jamii,” alieleza Mhe. Jaji Mkuu.

 

 

Akizungumza katika mahojiano maalum mara baada ya kuapishwa, Mhe. Banza ameahidi kutumikia vyema nafasi hiyo kwa kufuata misingi ya sheria na taratibu zilizopo katika kutekeleza majukumu yake ya uhakimu.

 

 

Akizungumzia safari yake ya utumishi ndani ya Mahakama Mhe. Banza amesema, alianza kufanya kazi Mahakama kama Karani wa Mahakama ya Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro mwaka 2004.

 

Mwaka 2006, Mhe. Banza alihamishiwa Mahakama ya Rufani, Kitengo cha Masjala ya wazi akihudumu kama Karani wa Mahakama hiyo. Mnamo mwaka 2008 alihamishiwa Mahakama Kuu ya Tanzania- Dar es Salaam, Kitengo cha Jinai akihudumu kama Karani wa Mahakama hiyo.

 

Aidha Mhe. Banza  ameendelea na kazi hiyo ya Ukarani hadi kuapishwa kwake rasmi leo Aprili 25, 2019.

Akizungumzia safari yake ya masomo, Mhe. Banza amesema alianza kujiendeleza kimasomo mwaka 2007 katika fani ya Sheria mpaka alipohitimu mwaka 2011 katika Chuo Kikuu Huria-Dar es Salaam. Mwaka 2014 Mhe. Banza alijiunga na Shule ya sheria (Law School) na kufanikiwa kuhitimu masomo yake ya uanasheria kwa vitendo.

 

 

Hafla hiyo fupi imehudhuriwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi pamoja na Maafisa kadhaa wa Mahakama ya Tanzania.

 

 

Na Mary Gwera na Dennis Buyekwa, Mahakama

 

 

Comments are closed.