The House of Favourite Newspapers

Mahakama ya Tanzania Yaongeza Nguvu’IJA’ Matumizi ya Tehama

0
d

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema kuwa, Mahakama ya Tanzania kupitia awamu ya pili (II) ya Mradi wa Uboreshaji huduma wa mwaka 2021-2025 unaofadhiliwa na Benki ya Dunia (WB) imetenga jumla ya Dola milioni 6 katika eneo la kuongeza mafunzo ya kuongeza Ujuzi (Skills) na Maarifa (knowledge) kwa watumishi wa Mahakama sambamba na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

Akizungumza na Wahitimu wa Astashahada na Stashahada ya Sheria pamoja na wageni waalikwa katika Mahafali ya 22 ya Chuo hicho leo tarehe 07 Desemba, 2022, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Juma amesema kuwa, lengo ni kuhakikisha Chuo hicho kinachotoa elimu na mafunzo kwa wanafunzi wake na kwa watumishi wa Mahakama kwa njia ya TEHAMA.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Ibrahim Hamis Juma (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wahitimu wa Stashahada ya Sheria kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

 

Kutengwa kwa kiasi hicho kikubwa cha fedha katika Mradi huu wa pili ni ushahidi kuwa, Chuo kinatakiwa kuhama kutoka ‘analogue’ hadi kidijitali katika utoaji wa mafunzo. Fedha zilizotengwa sio za Semina na Makongamano, ni za Maboresho ambayo yatatoa matokeo, yatakayopimika na yatakayotathminiwa (evaluated) na Serikali ya Tanzania na Maafisa wa Benki ya Dunia, hivyo ni muhimu kuchangamkia nafasi hii,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Prof. Juma amesema kwamba, Chuo cha Uongozi wa Mahakama kinatakiwa kitengeneze Jukwaa la Ki-elektroniki ‘e-learning platform’ litakalotumia akilibandia (Artificial Intelligence) kwa ajili ya kufundishia, na wanafunzi kupata mafunzo kwa njia ya mtandao.

Ameongeza kuwa, jukwaa hilo linatakiwa liwe la kisasa na lenye ubora, na liweze kutumika kutoa elimu na mafunzo sio tu kwa wanafunzi wa Stashahada na Astashahada ya Sheria, bali pia litumike kutoa masomo na mafunzo Elekezi na Endelevu kwa Majaji, Wasajili, Naibu Wasajili, Watendaji, Mahakimu na Watumishi wa kada zote.

Ni mategemeo yetu kuwa, Jukwaa hilo litasheheni taarifa na mambo yote muhimu ambayo wanafunzi, wahadhiri na watumiaji wengine watajisomea na kujiendeleza: “Support for the launch of the IJA’s e-learning platform and courses and for the use of AI tools for state of-the-art trainee experience and use by judges, 11 magistrates, and newly employed Judges, Magistrates, Registrars, Administrators and Staff.” Baada ya kuwekeza katika Jukwaa (e-learning platform) Chuo hiki hakitakuwa kisiwa, kitapata wanafunzi dunia nzima na kuwawezesha watumishi walio kazini kuendelea na kazi huku wakisoma,” ameeleza Jaji Mkuu.

Amesema kuwa, Jukwaa la Ki-elektroniki litakalotengenezwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama kwa ajili ya kutoa mafunzo (e-learning platform), litasaidia kuokoa muda kwakuwa litatumika kutoa mafunzo katika majengo Jumuishi yaliyojengwa na yatakayojengwa na Mahakama na ambayo yatatumika pia kama vituo vya mafunzo kwa njia ya teknolojia kwa watumishi na wadau bila kusafiri hadi IJA Lushoto.

Amewasihi Wahadhiri, Wakufunzi na Watumishi wote wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, kujitayarisha na matumizi ya Jukwaa la Ki-elektroniki (e-learning platform) kutoa mafunzo na elimu sio tu kwa wale waliopo ndani ya Kampasi hiyo, bali hata wale walio nje ya Kampasi Chuo“Mkifanikiwa kutekeleza matarajio ya Mradi wa Maboresho ya Mahakama kwa kusanifu upya Stashahada ya Sheria, Astashahada ya Sheria, na mafunzo Elekezi na Endelevu, mtakuwa mmetoa mchango mkubwa katika kuboresha Elimu ya Sheria Tanzania,” amesisitiza.

Kwa upande wa Wahitimu, Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Juma amewaeleza kuwa, Watanzania wa leo wanaishi katika dunia inayosukumwa na Teknolojia yenye nguvu kubwa ya Mapinduzi ya Nne ya Viwanda (4th Industrial Revolution). Hivyo, wahitimu wote wenye elimu ya ngazi au daraja lolote ni lazima wahakikishe kuwa elimu waliyopata kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama haitoshi na ni lazima waiboreshe kila siku ili ilingane na mahitaji ya ushindani mkubwa katika Karne ya 21.

Mbali na kuweka msisitizo kwenye TEHAMA, Mhe. Prof. Juma aliyekuwa Mgeni rasmi kwenye Mahafali ya Chuo hicho, amewaasa Wahitimu wote kuwa waadilifu, nidhamu ya kweli na sio ya woga, bidii na wenye ujuzi wa kutosha, uwezo wa kiuongozi kuanzia ngazi ya familia hadi kitaifa na kuwa wanajamii wema na kuitumikia vyema jamii.

Nawaomba wahitimu wote kutambua kuwa siku zote elimu uliyonayo huwa haitoshi. Kasi ya maboresho na Mabadiliko ya Elimu inatakiwa ilingane na Kasi ya Mabadiliko ya Mahitaji ya Jamii husika kwa kuzingatia uadilifu na nidhamu ya kweli katika kazi,” amesema Jaji Mkuu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani (T), Mhe. Dkt. Gerald Ndika amesema kuwa, Chuo hicho kimepata mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na kukamilisha utayarishaji wa Mwongozo wa Ufundishaji wa ajili ya Watunza Kumbukumbu wa Mahakama kuhusu Uendeshaji wa mashauri ya Watoto (Training Guide for Record Management Assistants on Handling Juvenile Cases).

Mhe. Dkt. Ndika ameongeza kuwa, Chuo hicho kimeweza kufanya mafunzo elekezi kwa Majaji wa ngazi zote pamoja na kwa watumishi wapya wa kada zote za Mahakama kitu ambacho ni hatua kubwa katika kujenga uwezo katika utendaji kazi.

Naye, Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama na Jaji wa Mahakama ya Rufani (T), Mhe. Dkt. Paul Kihwelo ameeleza kwamba, katika mahafali hayo jumla ya wanafunzi 574 wamehitimu masomo yao, ambapo kati yao 289 ni wa kike na 286 ni wa kiume. Wahitimu wa Astashahada ya Sheria (NTA Level 4) ni 348 na wa Stashahada ni 226. Idadi hii inafanya jumla ya wahitimu wa Chuo hicho kufikia leo kuwa 1,148.

Kabla ya kushiriki katika mahafali hayo, Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Juma alizindua bweni la wavulana wanaosoma katika chuo hicho. Wageni wengine waliohudhuria katika mahafali hayo ni Mhe. Dkt. Benhajj Masoud, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo (LST), Mhe. Dkt. Juliana Masabo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu, Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, Mhe. Frederick Manyanda, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Lushoto, Wahadhiri na Watumishi cha Chuo cha IJA, wazazi pamoja na wageni wengine waalikwa.

 

Na Mary Gwera, Mahakama-Lushoto

Leave A Reply