The House of Favourite Newspapers

Majaliwa: Nyumba za ibada zihamasishe amani

majaliwaaaWaziri mkuu mh. Kassim Majaliwa

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewaomba viongozi wa dini zote kutumia nyumba za ibada kuwahamasisha waumini umuhimu wa kulinda na kudumisha amani na utulivu uliopo nchini.

Amesema Serikali itahakikisha amani na utulivu vinaendelea kudumishwa ili Watanzania wawe na uhakika wa kuendelea kufanya kazi zao za kuwaingizia kipato na kuwaletea tija.

Majaliwa alitoa wito huo jana alipozungumza na waumini wa kiislam baada ya kumaliza kuswali sala ya Eid El Haji kwenye viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke, Dar es Salaam.

“Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo yote nchini. Wito wangu kwa viongozi wa dini msisitize waumini juu ya utunzaji wa amani na kukemea vitendo viovu Taifa lizidi kusonga mbele,” alisema.

  Waziri Mkuu pia aliwasisitiza wananchi kuendelea kuwaombea mahujaji waliopo Makka na Madina, Saudi Arabia wakiendelea na ibada ya hijja, warudi salama.

Vilevile, alitumia fursa hiyo kuwaomba wananchi kuwasaidia kwa hali na mali watu waliokumbwa na tetemeko la ardhi mkoani Kagera ambako   watu 16 walifariki dunia na wengine 253 kujeruhiwa.

Awali akisoma hutuba ya Eid, Sheikh Nurdin Kishki alisema Uislamu ni dini ya amani hivyo amewaomba waislamu kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani yakiwamo mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.

Sheikh Kishki alisema ni muhimu watu kulinda amani kwa sababu  ikitoweka ni vigumu kuirudisha.

Alitoa  mfano wa Libya na Misri ambazo hadi sasa zimeshindwa kuirudisha amani.

CREDIT: MTANZANIA.

 

Comments are closed.