MAJANGA! Jumla ya familia zipatazo saba wiki moja iliyopita zilijikuta katika wakati mgumu kufuatia kubomolewa kwa nyumba waliyokuwa wakiishi, kufuatia mke mdogo wa mmiliki wake, kufika na kubomoa jengo hilo baada ya kushinda kesi ya mzozo wa kifamilia mahakamani.
Breaking News: Jambazi Aliyeongoza Mauaji ya Polisi 8 Kibiti Auawa -Dar
Tukio hilo la kusitikitisha lilitokea Septemba 5 mwaka huu huko Mtaa wa Mtongani Kunduchi jijini Dar ambapo familia hizo zilianza maisha mapya ya kupigwa na jua, mvua na baridi nje, huku baadhi yao wakipoteza mali na fedha kufuatia mama huyo kufika eneo hilo akiwa ameandamana na katapila na mabaunsa, bila hata kutoa notisi kwa wapangaji wake.
Kwa mujibu wa mtoto wa kwanza wa mmiliki wa nyumba hiyo ambaye hivi sasa ni marehemu, aliyetambuliwa kwa jina moja la Robert, alisema mzozo wa kugombea mali hizo ulianza mara tu baada ya kufariki kwa baba yake aliyekuwa na wake wawili, huku mkubwa akiwa naye ametangulia mbele za haki.
“Baada ya kifo cha baba yetu, tulibaki na mama yetu mdogo, tukiwa jumla ya watoto watano, yeye aliishi kwenye mji wake akiwa na wanaye watatu, na mimi na mdogo wangu tukabakia kwenye nyumba hii (iliyobomolewa) hata hivyo siku chache baadaye mama akatutaka tuhame akidai nyumba hii ni yake aliachiwa urithi na baba yetu.
“Hatukuwahi kuwa na ugomvi wowote na mama yetu huyo, kwa kweli tulishangaa sana, tulipokataa akaamua kutupeleka mahakamani, akisema eti tumemdhulumu mali za mumewe, mambo yale yalikwenda harakaharaka mno, ukweli ni kwamba alitushindwa kesi, mali hizi akakabidhiwa yeye kama mwangalizi mkuu. Siku chache baadaye akatuletea ujumbe akitutaka tuhame akisema anataka kubomoa na kuuza eneo hili,” alisema Robert.
“Baada ya nyumba kubomolewa tumejikuta tukikosa pa kuishi, mali na fedha zetu zimepotea, usalama wetu na watoto wetu umekuwa mdogo mno, hadi sasa hatujui kesho yetu ni nini” alimaliza Godfrey.
Risasi Mchanganyiko lilimtafuta mama huyo aliyejulikana kwa jina moja la Roda, lakini hakuweza kupatikana, ingawa Mwenyekiti wa Mtaa huo, Tabu Athuman, alikiri kuusikia mgogoro wa familia hiyo kwa muda mrefu.
ALLY KATALAMBULA, RISASI MCHANGANYIKO.