Mkuu wa Utawala Jeshi la Polisi nchini, Naibu Kamishna (DCP), Lucas Mkondya leo amemuwakilisha Inspekta Jeneral (IGP), Simon Sirro kutembelea ofisi za Global Group.
DCP Mkondya ambaye aliongozana na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Lazaro Mambosasa amevipongeza vyombo vya habari vinavyomilikwa na Makampuni ya Global Group kwa kazi kubwa wanaoifanya ya kuuhabarisha umma na kuibua matukio mbalimbali ya uhalifu.
Aidha, makamanda hao wamesema matukio mengi yaliyoibuliwa na vyombo vya habari vya Global wameyafanyia kazi na kuwakomboa waliokuwa wakitaka kudhulumiwa au kupoteza haki zao na kuwatia hatiani wahalifu wa makosa hayo.
“Tunavipongeza sana vyombo vya habari vya Global, tumekuwa tukiwafuatilia sana, mnafanya kazi kubwa na sisi tumekuwa tukiwapa ushirikiano wa kila namna. Licha ya kwamba tumehamia Dodoma lakini hamjasita kutualika.
“Tunaomba kila mmoja wetu ahakikishe katika eneo lake anailinda amani ya nchi hii. Watu waishi kwa kufuata sheria, raia mwema haguswi na jeshi la polisi,’ amesema.
Aidha, akizungumzia kuhusu mauaji yaliyotokea Tandahimba mkoani Mtwara mwishoni mwa mwaka jana, DCP Mkondya amesema mauaji hayo yalisababishwa na kikundi cha wahuni waliotoka Kaskazini mwa Msumbiji na kuja kufanya uhalifu nchini.
“Wengi wao ni wale waliokuwa wakifanya uhalifu pale Kibiti mkoani Pwani, baada ya kuwapiga na kuwatimua, walikimbilia Kaskazini mwa Msumbuiji, lakini tumejipanga kuthibiti matukio haya ya kihuni ili yasifanyike tena,” amesema Mkondya.
Aidha, akizungumzia kuhusu polisi kukiuka maadili na kujihusisha na vitendo vya utakatishaji fedha, Kamanda Mkondya amesema Jeshi la Polisi halitowaacha salama.
“Hawa hatutawaacha, wote tutawafukuza, hawawezi kulipaka jeshi letu matope tukawaacha, jeshi letu lipo vizuri. Hata wananchi wanaojifanya ni viongozi wa Serikali kugushi na kuiba pesa, tunawaambia wafanye kazi nyingine, tutawakamata.
Kwa upande wake Kamanda Mambosasa alipoulizwa kuhusu viongozi wa Jeshi hilo kutofautiana katika kutoa taarifa kwa wananchi kama ilivyotokea kwa tukio la kukamatwa kwa mfanyakazi wa Kituo cha cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Tito Magoti, amesema; “Jeshi la Polisi tunao mfumo mzuri sana wa mawasiliano, kuanzia chini mpaka juu, na huu mfumo umewekwa na upo kwenye maandishi. Nikitoa tamko linawabana waliochini yangu.
“Kilichotokea ni ajali kwa Kamanda wa Kinondoni, alikuwa hajasoma kile nilichokizungumza, akajikuta anaongea kama anapingana na kile nilichokisema, lakini siku hiyo hiyo alipokanusha mtuhumiwa hajakamatwa ndipo alikuwa akifikishwa mahakamani hivyo kauli yangu ikabaki hivyo hivyo.
Aidha, makamanda hao wamewashukuru wananchi kwa kushirikiana na jeshi la polisi kufichua mambo mbalimbali ya uhalifu na kuhakikisha wavunjifu wa amani wanakamatwa na kuwafikisha kwenye vyombo vya haki ili sheria ichukue mkondo wake.
Ā
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL Ā