UKATILI wa kutisha! Hakuna lugha nyingine unayoweza kuzungumza zaidi ya kusema hivyo, baada ya mama mmoja, mkazi wa Sinza C jijini Dar es Salaam, kukata uume wa mtoto wa jirani yake, kwa madai kuwa alimbaka binti yake wakati wakicheza sebuleni, Risasi Jumamosi limetonywa.
Inadaiwa kuwa mtoto aliyepatwa na maswaibu hayo, Richard mwenye umri wa miaka minne, alikuwa sebuleni akicheza na binti aliyefahamika kwa jina moja la Abby (3) kabla ya mama mwenye nyumba kurejea na kushangaa kumuona bintiye akiwa na tone la damu kwenye nguo zake.
Akizungumza na paparazi wetu, baba wa Richard, Paul Konyaki alisema alipewa taarifa na majirani wa mtaa wa pili siku chache zilizopita kuwa mtoto wake amekatwa sehemu za siri na mama huyo.
“Huyo mama alipotoka kazini alimkuta mtoto wake ana tone la damu kwenye nguo, ndipo akaanza kumbana mtoto wangu kamfanya nini mwenzake na kuanza kumuadabisha kwa kumkata na kisu sehemu ya mbele ya uume wake akidai kambaka mwanaye.
“Ni kitendo ambacho kilinistaajabisha maana wale wote ni watoto na aliwakuta wamekaa tu, si kwamba aliwashuhudia wakifanya uchafu na nyumba hiyo ilikuwa na dada wa kazi, sasa kama kuna utundu ulifanyika hadi yule mtoto kuumia akatoka damu, si angemsikia akilia, lakini haikuwa hivyo,” alisema.
Akiwa na jazba, baba huyo alisema, jambo hilo lilimkera kwani ni ukatili uliokithiri, hivyo akaanza kuhaha kutafuta anapoishi na akafanikiwa kupajua kwa msaada wa majirani ambao wanamfahamu.
“Nilipofika pale badala awe mpole kwa ukatili alioufanya, akaanza kunitambia kuwa yeye anafanya kazi serikalini, siwezi kumfanya chochote na kunilaumu kuwa sijamlea vyema mwanangu, nikaona huyu atanisababishia matatizo mengine, nikaachana naye.
“Nikaenda polisi kuchukua PF3 kisha nikaenda Hospitali ya Palestina ambapo madaktari walishauri wamfanyie tohara kabisa kutokana na hali aliyokuwa nayo ili kumnusuru tatizo lisiwe kubwa zaidi, taratibu za kisheria zinaendelea hadi tufikishane mahakamani,” aliongeza.
Kwa upande wake, mtoto huyo aliyefanyiwa unyama huo alisema; “Mama yake alivyorudi kazini alitukuta tunaangalia katuni akaanza kunifinya na kunikata huku na kisu, yule baba yake Abby akasema msamehe yeye hataki, akaniambia wee usije tena kucheza na mtoto wangu.”
Risasi Jumamosi lilimtafuta mwanamke huyo kwa njia ya simu, lakini namba yake haikuweza kupatikana hewani, lakini alipopatikana mumewe, alisikiliza tuhuma hizo mwanzo mwisho na alipotakiwa kusema chochote, alikata simu.
Shauri hilo limeripotiwa katika Kituo cha Polisi Mabatini (Kijitonyama) na kuandikiwa jalada lenye namba KJN/RB/6258/17 SHAMBULIO 08/06/17.j
STORI: MAYASA MARIWATA, RISASI JUMAMOSI