The House of Favourite Newspapers

Mambo Matatu Yaliyomng’oa Wema Chadema Yafichuka!

Wema Sepetu.

SIKU chache baada ya mrembo wa Bongo Movies, Wema Sepetu kurejea Chama Cha Mapinduzi (CCM), imebainika yapo mambo matatu yaliyomsababisha mrembo huyo arejee na kuachana na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Kabla ya kufanya uamuzi huo Ijumaa iliyopita, Wema na mama yake mzazi, Miriam Sepetu, waliokuwa makada wa CCM, Februari 24, mwaka huu, walitangaza kujiunga na Chadema wakidai wanaifuata demokrasia ya kweli.

 

Hata hivyo, mama wa mrembo huyo, aliitisha mkutano wa waandishi wa habari na kusema yeye hana mpango wa kurejea tena CCM na atamalizia maisha yake duniani akiwa Chadema.

Chanzo kilicho karibu na Wema, kimeeleza kuwa, mambo ambayo yamemfanya mrembo huyo arudi CCM ni pamoja na lile alilolianisha mwenyewe wakati alipotangaza kurejea chama hicho tawala.

“Jambo la kwanza kabisa ni amani ya moyo. Kama ulivyosikia siku ile alipotangaza kurudi CCM alisema kabisa hana sababu ya kubaki kwenye chama ambacho hakimpi amani ya moyo. Amerejea CCM ambako alikuwa anaipata,” kilisema chanzo hicho.

 

Ukiachana na hilo, chanzo hicho kiliweka bayana kuwa, jambo lingine lililomsababisha mrembo huyo arejee CCM ni kitendo cha kuwaona viongozi mbalimbali wakubwa wakijiunga au kurejea CCM.

“Wema aliamini kwamba viongozi aliowakuta, kina Lawrence Masha na wengineo wangeendelea kushikamana na kujenga chama lakini matokeo yake wimbi la wanaharakati wengi wa Chadema kukikimbia chama hicho limeongezeka,” kilisema chanzo hicho.

 

Aidha, chanzo hicho kililitaja jambo lingine lililosababisha Wema arejee katika chama hicho tawala ni pamoja na kutokabidhiwa kadi ya Chadema kwa muda mrefu.

“Unajua aliona kama anakosa zile confidence za kujinasibu kama ni Chadema damu. Hilo limemfanya aone kuna urahisi tu yeye kutoka kwani anakokupigania wala hakujamfunga kivile,” kilisema chanzo hicho.

 

Pamoja na hayo matatu, vyanzo vingine vimeeleza kuwa mrembo huyo amerejea CCM kwani kuna fursa za kazi mbalimbali ambazo anaweza kunufaika nazo tofauti na akiwa nje ya chama hicho.

Taarifa nyingine kutoka ndani ya familia zimeeleza pia, huenda baadaye mama wa mwingizaji huyo pia akamfuata mwanaye licha ya mwenyewe kukaririwa akisema kuwa hana mpango huo.

 Stori: MWANDISHI WETU, Dar.

MAGAZETI TANZANIA: MAMBO MATATU YALIYOMNG’OA WEMA CHADEMA YAFICHUKA

Comments are closed.