Man United na Ronaldo Wafikia Makubaliano ya Pamoja ya Kuvunja Mkataba
KLABU ya Manchester United pamoja na mshambuliaji Cristiano Ronaldo wamefikia makubaliano ya pamoja ya kuvunja mkataba na kumfanya mchezaji huyo kuwa huru wakati akiwa anaendelea na majukumu yake akiwa na Timu ya Taifa ya Ureno kwenye mashindano ya Fainali za Kombe la Dunia nchini Qatar.
Taarifa ya kuvunjwa kwa mkataba huo imethibitishwa na tovuti ya klabu ya Manchester United ambayo imebainisha kwa kina kuwa utekelezwaji wa makubaliano hayo unaanza mara moja.
“Cristiano Ronaldo anaondoka mara moja, Manchester United kwa makubaliano ya pande zote mbili.”
Klabu inamshukuru kwa mchango wake mkubwa katika nyakati zote mbili Old Trafford akifanikiwa kufunga mabao 145 katika michezo 346 na tunamtakia yeye na familia yake mafanikio katika Maisha yake ya baadaye.” Taarifa kutoka Manchester United.
Kwa upande wake Cristiano Ronaldo ametoa taarifa iliyosema:
“Kufuatia mazungumzo na Manchester United tumekubaliana kwa pamoja kuvunja mkataba wetu mapema.
Naipenda Manchester United, nawapenda na mashabiki, hilo haliji kubadilika kamwe. Lakini nadhani kwa sasa ni wakati wangu kutafuta changamoto mpya ya maisha, naitakia timu mafanikio kwa kipindi kilichobaki cha msimu na baadaye.”
Kinachosubiriwa kwa hamu ni kuona Cristiano Ronaldo atatimkia katika klabu gani kufuatia kuachana na Manchester United je anaweza kubaki Barani Ulaya, kuelekea Saudi Arabia au Kwenda katika Ligi Kuu ya Marekani MLS?.