Mane Apiga Bao la 100 Liverpool
KOCHA wa Liverpool, Jurgen Klopp amesema anafurahi sana kuona anamfundisha mshambuliaji mahiri kama Sadio Mane.
Mshambuliaji huyo juzi alifanikiwa kufunga bao lake la 100 akiwa na Liverpool kwenye mchezo wa Ligi Kuu England dhidi ya Crystal Palace.
Liverpool wakiwa kwenye kiwango cha juu juzi walifanikiwa kupata ushindi wa mabao 3-0 kwenye mchezo huo.
Klopp amesema anaona fahari kubwa sana kwake kumfundisha mshambuliaji huyo mwenye kiwango kikubwa zaidi duniani kwa sasa.
Mane amefikisha mabao hayo baada ya kutumika kwenye michezo 224 ya Liverpool.
“Sadio amefanikiwa kufunga mara yake ya tisa kwa kipindi chote alichokutana na Palace, lakini hili ni bao lake la 100 akiwa na Liverpool.
“Hili ni jambo zuri sana na la kuvutia na kwangu ni fahari kubwa kuona kuwa ninamfundisha mchezaji wa aina yake, ni mara chache sana hutokea.
“Mabao 100 ni kama namba tu lakini ukweli ni kwamba ninafuraha sana kuwa naye,” alisema Klopp.
LIVERPOOL, England