Mapazia Ya Chumbani -8
ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:
Mama Kirumba akavuta pumzi kwa nguvu kisha akazitoa na kumwangukia mzee Mashali huku akisema…
“Tumeshaamua kumla nguruwe, basi tumle aliyenona tu.”
ENDELEA NAYO MWENYEWE…
Si mzee Mashali wala mama Kirumba wote walibaki wameduwaa kwa muda mrefu mle chumbani hali iliyowafanya washindwe hata kuendelea na ungwe ya pili.
“Baba Dick,” aliita mama Kirumba.
“Nakusikia.”
“Mimi nina wazo.”
“Lipi hilo.”
“Yaani najua tu mkeo pamoja na mama Muro wapo pamoja hivi sasa na ndiyo chanzo hata cha wote kuja na mada hiyohiyo. Cha msingi niwafuate na kuwavuruga.”
“Hapana, hapana! Uwavuruge?”
“Si kuwavuruga kwa kuwapiga.”
“Ila?”
“Yaani nijifanye sijui lolote, nikifika hapo nawatungia uongo wowote utakaofanya niondoke nao na kwenda nao nje ya kwako halafu huku nyuma wewe unaondoka kiulaini unarejea kwako.”
Mzee Mashali alilifikiria wazo hilo kwa sekunde kadhaa, akalipima kama linawezekana.
“Mama Kirumba!”
“Abee!”
“Una akili sana wewe,” alisema mzee Mashali huku akiuchukua mkono wake na kushika mapaja ya mama Kirumba.
“Kwa hiyo nijiandae niende basi.”
“Nenda lakini ufanye kwa machale maana wasije kushtukia utachokifanya.”
Mzee Mashali alishusha pumzi huku macho yake yakisindikiza kuangalia umbo la mama Kirumba kwa jinsi alivyoumbika.
“Sijui nikaoge kabisa.”
“Ukaoge tena! Watashtukia, nenda hivyohivyo tu.”
“Ujue sisi wanawake tukitoka kwenye hali kama hizi ni rahisi kujuana wenyewe kwa wenyewe, isitoshe mama Mashali ni mwanamke aliyefundwa akafundika, atanigundua tu kama nitaenda hivihivi bila kujisafisha.”
* * *
Mama Mashali alirudi nyumbani kwake akiwa amenyong’onyea mithili ya kifaranga kilichomwagiwa maji. Nguvu zilimuisha na kuanza kuamini kidogo huenda kweli mumewe ambaye ni baba Dick hayupo chumbani kwa mama Mashali.
“Vipi tena shoga kulikoni, umemuona?” aliuliza mama Muro baada ya mama Dick kurejea.
“Nimuone wapi?”
“Lakini mama Dick, kuna kitu nyuma ya pazia na za mwizi arobaini na kama siyo leo basi zitakuwa zinakaribia kufika hiyo arobaini.”
“Kweli mama Muro lakini sasa, ujue bado siamini amini, ni huyuhuyu mama Mashali ananifanyia mchezo mchafu tena mazingira hayahaya?”
“Mi nina wazo?”
“Wazo gani tena mama Muro?”
“Twende kwa mjumbe na kumuelezea haya mambo huenda akatupa njia sahihi au hata kuvamia kwa mama Mashali na akaumbuka.”
Kama kawaida ya mama Muro kwa ulopolopo. Alimshawishi mama Dick lakini bado somo hilo lilikuwa halijamuingia vizuri akilini.
“Na kama tutamuhakikishia mjumbe kuwa baba Dick yupo ndani halafu tunakaingia hayupo, ujue hiyo ni aibu mama Muro?”
Wakiwa bado katika maongezi, mara ghafla wakamuona mama Kirumba akitoka nyumbani kwake.
“Haya sasa kumekucha, ona?” alisema mama Muro baada ya kumuona mama Kirumba.
Hapohapo mama Dick akalegea huku mkono wake mmoja akiunyoosha kuelekea kwenye miguu ya mama Kirumba aliyekuwa ameshafika katika eneo hilo.
* * *
Mzee Mashali presha ilikuwa juu tena kwa muda. Alikuwa sebuleni kwa mama Kirumba huku akichungulia dirishani muda wote kuangalia eneo la nyumbani kwake endapo atamuona mkewe, mama Muro pamoja na mama Kirumba wakiongozana ili aweze kuchomoka.
Ghafla macho yake yakakutana na wote hao aliokuwa akiwafikiria lakini wakiwa katika purukushani ambapo mkewe alikuwa chini ameshikwa mikono.
“Vipi tena?” alijisemea kimoyomoyo.
“Au mama Kirumba ameshaharibu nini?”
Kwa hofu, baba Dick alielekea chumbani kwa mama Kirumba na kuchukua suruali yake kisha akaitumbukiza kwenye mwili na kufunga mkanda vizuri halafu akaenda sebuleni lakini ghafla kuangalia chini sendozi zake hakuziona.
“Sasa atakuwa ameweka wapi huyu mama Kirumba?”
Akatafuta huku na kule lakini hakuziona, ikabidi awe mdogo kwa kukaa na kuendelea kutizama moja kwa moja kinachoendelea kati ya mkewe, mama Kirumba pamoja na mama Muro.
Mzee Mashali akiwa katika kuwaza na kuwazua bila kujua atatoka na viatu gani mle ndani, ghafla jicho lake likatazamana na sendozi za kijani zikiwa zimenyanyuliwa juu na mama Muro. Hakutaka kuamini macho yake.
“Ina maana mama Kirumba alienda na sendozi zangu?”
Je, nini kiliendelea hapo? Usikose chombezo hili wiki ijayo.