The House of Favourite Newspapers

Mapenzi yana maumivu lakini yanasahaulika !

0

Ni wiki nyingine mpenzi msomaji wa safu hii ya XXlove tunakutana tena jamvini hapa kwa neema na rehema za Mwenyezi Mungu. Leo tunaangalia ni kwa namna gani mapenzi yanaweza kuwa sumu kali inayosambaa kwa haraka sana katika miili ya wanadamu wa jinsi zote.

Ni kweli kwamba, mapenzi yanatesa kuliko kitu chochote katika uso wa dunia hii. Ni mapenzi hayohayo ambayo yana nguvu na maumivu makali kuliko maumivu ya kitu chochote unachokijua chenye kusababisha maumivu.

Pia ni kweli wapo watu wengi wameumizwa na kuteswa na mapenzi. Wengine wanaendelea kuteseka na kuumia kila siku. Wengine wanatamani kuyaepuka ingawa hawawezi zaidi ya kupumzika kwa muda. Wapo wanaotamani kuyakimbia ila hayakimbiliki. Wengine wanatamani kujiua ila roho wa Mungu anawashindia.

Inawezekana ni kweli mpenzi wako amekuumiza sana lakini vumilia kwani maumivu hayo ni ya muda na ninaamini ipo siku utayasahau.

Maumivu unayoyapata kwa sababu ya mke, mpenzi, mchumba au mume wako ni ya mpito tu, ni kama masika na kiangazi kinavyoikumba ardhi, mara nyingi huwa ni kwa mpito.

Kuna msemo ambao hutumika sana katika dunia tuliyonayo usemao ‘hakuna marefu yasiyokuwa na ncha’. Hakika maneno haya yana ukweli f’lani ndani yake na ndivyo ilivyo kwamba, mapenzi yanaumiza, yanatesa, yanasumbua ila maumivu yake yana mwisho. Haijalishi umeumia, umeteswa kwa muda au namna gani lakini amini siku yaja nawe utapona na kurudi katika hali yako ya zamani.

Usimchukie aliyekuumiza na kukutesa katika mapenzi, amini ni sehemu ya maisha yako, ulipaswa kuyapita.

Wapenzi wengi wamekuwa wakiteseka mno na namna ya kuwasahau wenza wao baada ya kutengena au kuachwa. Baada ya mada ya wiki iliyopita nilipokea simu ya msomaji wangu kutoka jijini Mwanza akilalamika kuwa ameachana na mpenzi wake aliyedumu naye kwa miaka minne lakini kinachomtesa akilini mwake ni fikra na mapenzi juu ya mpenzi wake huyo.

KIMSINGI IKO HIVI;
Kwa sababu ya mazoea na kushirikiana katika masuala au vitu vingi na mpenzi wako ndiyo maana huwa ni vigumu sana kumsahau lakini baada ya muda naamini unaweza kusahau. Kipindi cha maumivu ya mapenzi ni kama kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu ambapo kila mtu anatamani chama chake kishinde na kama kipindi hiki cha uchaguzi kikitumika vibaya na kusababisha uvunjifu wa amani, basi wananchi wa nchi husika watakuwa wamekosa busara kwani uchaguzi ni suala la mpito na ndivyo ilivyo kwa maumivu ya mapenzi, huwa ni suala la mpito tu.

Tukutane wiki ijayo. Pia usikose kutembelea ukurasa wetu wa Mimi na Uhusinao kwenye Mtandao wa Facebook kujifunza mambo mengi kuhusu mapenzi.

Leave A Reply