The House of Favourite Newspapers

MAPUTO KWENYE TUMBO LA SETH WA ESCROW, SIRI NZITO YAFICHUKA!

0
Harbinder Singh Seth.

 

BAADA ya Wakili Joseph Makandege anayemtetea mtuhumiwa wa uhujumu uchumi, Harbinder Singh Seth kuiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa mteja wake huyo yupo hatarini kufa kutokana na maputo aliyowekewa tumboni, siri nzito imefichuka, UWAZI linakupasha.

Wakili Makandege alidai mahakamani hapo wiki iliyopita kuwa mahakama ilitoa amri mara mbili ili mteja wake apelekwe Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili akatibiwe lakini magereza hawajatekeleza amri hiyo. Gazeti hili lilimtafuta Dk. Godfrey Chale ambaye amewahi kuhudumu katika hospitali mbalimbali jijini ikiwemo ya Muhimbili na Temeke na kumuuliza maswali kadhaa kuhusiana na tatizo linalosababisha mtu kuwekewa maputo tumboni, faida yake na athari zake, na kwa nini yanawekwa?

Akitoboa siri hiyo Dk Chale alisema maputo hayo yanawekwa tumboni kama tiba na yanaweza kukaa humo kwa muda mrefu, akafafanua kuwa maputo hayo yaitwayo kitaalamu intra-gastric balloon, ni laini sana na yanaweza kupasuka kirahisi kama mgonjwa hatafuatilia utaratibu wa uchunguzi wa mara kwa mara kuona kama bado yapo sawa na yametengenezwa kwa kutumia madini ya Silicon.

“Maputo huwekwa ndani ya tumbo la chakula na ndani yake huwekwa maji safi ya chumvi yaitwayo sterile salt au saline solution. Puto linapowekwa tumboni, hujaza nusu ya tumbo na muda wote aliyewekewa huhisi tumbo lake limejaa.

Kazi ya maputo haya husaidia kudhibiti hamu ya kula na kujikuta unakula kiasi kidogo sana cha chakula hivyo inakusaidia kudhibiti tatizo la kuongezeka unene kwa kasi,” alisema. Ili kupata undani wa maputo yanayowekwa tumboni, fuatana nasi katika maswali na majibu na Dk. Chale:

 

KWA NINI MTU ANAWEKEWA PUTO TUMBONI?

“Tiba ya kuwekewa puto inasaidia sana kudhibiti unene, ni njia ambayo siyo ya upasuaji, inapotumika pia husaidia kumuepusha mhusika kupata matatizo ya ini na figo. “Sababu za kuwekewa puto tumboni ni endapo mtu yupo katika hatari ya kupata magonjwa makubwa yanayohusiana na unene ambapo kitaalamu tunasema body mass index (BMI) yake inazidi 35 ambapo inaweza kumsababishia apate kisukari, ini kujaa mafuta, kupanda kwa shinikizo la damu, matatizo ya miguu na kwa mwanamke anapata vivimbe katika vifuko vya mayai au polycystic ovary syndrome.

“Mtu mwenye BMI zaidi ya 35 huwa ni mfupi na mnene sana. Mtu anaweza kuwekewa puto endapo tiba nyingine za kupunguza uzito au unene zimeshindikana, iwe kudhibiti ulaji au matumizi ya dawa za kupunguza unene kushindikana, na hawako tayari kupunguza unene kwa njia ya upasuaji.

 

PUTO LINAFANYAJE KAZI TUMBONI?

“Puto linapunguza nafasi tumboni hivyo inakusaidia ukila kidogo unahisi umeshiba. Mtu aliyewekewa puto anatakiwa ale chakula maalumu chenye kiwango kidogo cha nishati, awe mara kwa mara karibu na daktari wake, wauguzi na wataalamu wa lishe ili
kuhakikisha puto hilo linaendelea kuwepo bila tatizo.

 

NINI ATHARI YA KUWA NA PUTO TUMBONI?

“Mara nyingi watu wote waliowekewa puto huwa hawapati athari zozote na wanaendelea na maisha yao kama kawaida ila ni muhumu kuwa karibu na daktari wako kwa mawasiliano na endapo utahisi tatizo lolote basi toa taarifa kwa daktari wako, muuguzi wako au mtaalamu wa lishe.

“Hata hivyo, matatizo yanaweza kutokea mara chache sana inaweza kuumiza njia ya chakula kuanzia kinywani hasa wakati wa kuupitisha lakini ni jambo linalotibika wakati huohuo. Siku za mwanzo baada ya kuwekewa puto tumboni unaweza kujihisi vibaya tumboni, kichefuchefu na kutapika lakini haiendelei kwa muda mrefu.

“Kwa kuwa ni kitu kigeni tumboni, mwanzoni utahisi tumbo linakuwa zito, unacheua asidi mara kwa mara, maumivu ya mgongo na tumbo kujaa gesi lakini baadaye hali hiyo inapotea.

 

JE PUTO LIKIPASUKA TUMBONI INAKUWAJE?

“Athari mbaya inayoweza kutokea ni endapo puto hilo litanywea lote au kupasuka tumboni kwani husababisha puto hilo liende mbele na kuziba utumbo na tiba yake ni upasuaji wa dharura wa tumbo.

“Kama katika ufanyaji uchunguzi wa mara kwa mara itaonekana puto linaanza kunywea, au tunasema kitaalamu defleted, inamaanisha yale maji ya chumvi yanapungua taratibu, basi puto hilo itabidi litolewe kama lilivyowekwa.

“Kama umewekewa puto, basi hauruhusiwi kusafiri mbali na sehemu walipo wataalamu wako waliokuwekea na endapo itakulazimu usafiri, basi ni vizuri daktari wako akuruhusu na likitokea tatizo wasiliana naye mara moja ili afanye mawasiliano na daktari wa mahali ulipo.

 

JE PUTO LINAWEZA KUKAA TUMBONI KWA MUDA GANI?

“Muda wa puto kukaa tumboni na kuendelea kufanya kazi ni miezi sita hadi mwaka mmoja kutegemea na aina ya puto lililowekwa, maputo mengi hukaa kwa miezi sita halafu yananywea. “Endapo puto ni la miezi sita, basi lifuatiliwe na kutolewa kwa njia inayoitwa kitaalamu endoscopy. Njia ya kuyaweka huitwa Endoscopic Intragastric Balloon Insertion, na huwekwa tumboni puto moja hadi matatu na kama nilivyosema hukaa si chini ya miezi sita tumboni.

 

KUNA AINA NGAPI ZA MAPUTO HAYO YA TUMBONI?

“Aina za maputo haya ni nyingi kama vile Spatz, Orbera na Bio Enterics Intra-Gastric Balloon. NINI USHAURI WAKO? “Inashauriwa maputo haya yasikae tumboni kwa zaidi ya miezi sita ili kuepusha kunywea na kuleta madhara makubwa ikiwa ni pamoja na kupoteza maisha kama mgonjwa atachelewa tiba.”

 

YAPO MADAI KUWA KUNA UVIMBE MWINGINE TUMBONI KAMA PUTO, JE NI KWELI?

“Ni kweli tatizo hilo kitaalamu huitwa spasmodic pains, ni aina ya maumivu makali yanayohusisha mishipa ya fahamu na misuli. Maumivu haya yana tabia ya kuja kwa ukali na kupotea , ni maumivu ya kukata, yakitokea sehemu yeyote ya mwili lazima ukae na ushike sehemu hiyo.

“Spasmodic pains hutokea kwenye misuli ya miguu, ini, moyo, bandama, kongosho na tumbo. Ni maumivu yanayowatokea watoto na watu wazima. Zaidi maumivu haya hutokea tumboni sehemu yoyote lakini wengi hutokea upande wa juu wa tumbo na wanawake hutokea upande wa juu na hata upande wa chini kwenye kizazi hasa pale mwanamke anapokuwa kwenye siku zake, mimba kutishia kutoka na wakati mwingine anapokuwa katika kipindi cha upevushaji mayai au ovulation.

 

NINI TIBA YA TATIZO HILO?

“Tatizo la maumivu haya huchunguzwa hospitali kutegemea na sehemu yanapojitokeza. Pamoja na kutibu chanzo dawa za kutuliza maumivu haya zinaitwa Antispasmodic, pia zipo dawa za kupaka, kunywa na sindano,” alisema Dk Chale. Seth na James Rugemalira wanakabiliwa na mashitaka 12 ya uhujumu uchumi kwa kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu, kughushi nyaraka, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kutakatisha fedha na kuisababishia serikali hasara ya dola za Marekani 22,198, 544. 60 na Sh. 309, 461,300, 158.27. Wote wapo rumande Gereza la Segerea.

STORI: MWANDISHI WETU| UWAZI

Tambwe na Chirwa Waenguliwa Kikosini Yanga

Leave A Reply