The House of Favourite Newspapers

MARAFIKI, WANAJENGA, WANABOMOA UHUSIANO, JIFUNZE !

DUNIANI tunaishi kwa kutegemeana. Kwenye maisha kila mtu anamhitaji mwenzake kwa namna moja au nyingine. Anahitaji msaada wa mawazo, ushauri na hata fedha hivyo mtu huwezi kuepuka marafiki. Marafiki ndio ambao wanaweza kukupa msaada pale unapokuwa na uhitaji. Marafiki ndio wanaoweza kukupa faraja pale unapopitia kwenye kipindi kigumu. Ndio wanaoweza kukusaidia kwa hali na mali. Ndio wanaoweza kukuchangia pale unapokuwa na jambo lako mathalan, kitchen part, begipati, harusi na mambo mengine mengi.

Ili urafiki wowote ukue, unategemea sana wahusika kuwa na usawa. Wahusika wanapeana, staili ya nipe nikupe ndiyo inayodumisha uhusiano wowote ule. Ukitegemea kupewa kila siku na rafiki yako, lazima urafiki wako utasuasua tu. Hauwezi kuwa imara. Unaweza kujifanya mjanja kwamba uishi maisha yako, ukawa wewe unafanya mambo yako kwa siri halafu ya mwenzako unataka mshirikiane lakini mwisho wa siku lazima utajikuta tu umeaibika hivyo urafiki mzuri siku zote ni ule wa kushirikiana.

Urafiki unajengwa na upendo. Marafiki hawawezi kudumu kama ndani ya mioyo yao hawana upendo. Kila mmoja anapaswa kumpenda mwenzake kwa kiwango cha juu kabisa. Kila mmoja aguswe na matatizo ya mwenzake, kwenye shida na raha muwe pamoja. Siyo rafiki anakuwa na wewe kwenye furaha tu halafu linapokuja jambo la huzuni anakuacha peke yako. Anakuacha unapambana mwenyewe kuvuka tatizo husika, hakika mtu wa aina hiyo hawezi kuwa rafiki mzuri.

Kwenye uhusiano, suala la urafiki linapaswa kuchukuliwa kwa umakini zaidi maana mara nyingi marafiki ndio wamekuwa wakiharibu uhusiano. Marafiki ndio wanaosababisha maafa kwenye uhusiano wa watu. Wanafiki wanachochea ugomvi, marafiki wanaharibu kabisa uhusiano. Licha ya kuwa marafiki wanaweza kukusaidia katika uhusiano lakini inategemea ni rafiki wa aina gani na mwenye mawazo gani. Ni jukumu la kila mtu kuwatathimini marafiki zake na kuwatambua marafiki wazuri na wabaya.

Hili utafanikiwa tu kwa kuwapima mawazo yao, michango yao katika mambo yako. Inasisitizwa sana, kwenye masuala ya uhusiano, rafiki hapaswi kuchukua hatua kubwa sana ya kukuelekeza cha kufanya zaidi ya kukutia moyo wa uvumilivu pale unapokuwa kwenye kipindi kigumu.

Rafiki ambaye anakukatisha tamaa, rafiki ambaye hana ushauri mwingine zaidi ya kukuambia uachane na kila mpenzi unayeingia naye kwenye uhusiano na ukaingia kwenye ugomvi naye huyo si rafiki. Rafiki mzuri ni yule ambaye atakushauri pia kuhusu suala la uvumilivu. Rafiki mzuri atakueleza pia pale anapoona na wewe unakosea katika suala zima la uhusiano. Atakuelekeza kubadilika katika tabia ambayo anaona kabisa si nzuri na inaweza kukusababishia ukawa unagombana na kila mtu.

Unapaswa kuchagua marafiki wa kuwa nao maana si kila mtu anaweza kuwa rafiki yako. Ukaribu unatofautiana kati ya rafiki na rafiki. Kuna ambaye unaweza kumuweka karibu sana lakini kuna mwingine huna sababu ya kumuweka karibu. Siyo kila rafiki unayepaswa kumueleza kila kitu cha ndani. Lazima uwe unamuamini sana rafiki yako ndio umueleze mambo yako. Marafiki wengine badala ya kukusaidia, wanazidi kukuharibia. Hakikisha unakuwa una rafiki sahihi, ambaye siyo sahihi mweke pembeni.

Waswahili wanasema; ndege wanaofanana ndio wanaoruka pamoja hivyo kama unaona rafiki hamfanani tabia, mienendo basi huna sababu ya kuwa naye. Muepuke kama unaona ana sifa tofauti na wewe. Kwa leo inatosha, unaweza kunifuata kwenye mitandao ya kijamii. Instagram na Facebook natumia Erick Evarist, Twitter natumia ENangale.

Comments are closed.