HATIMAYE magari yenye kupaa yamewasili! Baada ya jitihada za kuunga mashine mbalimbali na kufanya majaribio kadhaa, Jeshi la Anga la Marekani, kwa kushirikiana na kampuni ya Lift Aircraft, wamefanya onyesho la gari la kwanza lenye uwezo wa kuondoka chini na kupaa moja kwa moja juu ambalo hutumia mota za umeme (eVTOL).
Onyesho la hilo gari hilo lililopewa jina la Hexa, limefanyika siku ileile ya kumbukumbu ambapo ndugu wawili wa Wright walipaisha ndege angani kwa mara ya kwanza miaka 112 iliyopita.
Tukio hilo lilienda sambamba na mpango wa kile kilichoitwa ukakamavu (Agility Prime) katika jeshi hilo, likimujuisha wabunifu, jamii mbalimbali na hata matukio yenye kulenga kuendeleza aina hiyo ya magari.
Likiwa na mashine 18 za rafadha (rotors), onyesho la Hexa lilifanyika huko Austin, Texas, mbele ya maofisa na watendaji wa kampuni la Lift. Hata hivyo, gari hilo lina uwezo wa kubeba mtu mmoja tu na kupaa moja kwa moja kwenda juu kutoka chini.
Taarifa za mwanzo zinasema, hakuna leseni maalum itakayohitajika kwa rubani kulipaisha, jambo ambalo ni dhahiri litazua migongano.
Zaidi ya hapo, kampuni ya Lift imesema italiuza Hexa kwa matumizi ya kawaida ya kiraia. Hata hivyo, kwa vile chombo hicho kimetengenezwa kwa ushirikiano na Jeshi la Anga, ni wazi kitafanyiwa majaribio zaidi ya kijeshi na hata kuongezewa zana mbalimbali kwa ajili ya majukumu mengine ya kijeshi.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa AFWERX, Coronal Nathan Diller, mpango wa Jeshi la Anga la Marekani kuhusu ubunifu, watengenezaji zaidi ya 15 wa ndege duniani wamevutiwa na teknolojia ya Hexa wakitaka kuitumia.
Haifahamiki lini Hexa itafika mitaani, lakini kwa kwa mujibu wa mpango wa Agility Prime na Lift, majaribio yataanza ifikapo mwaka 2023.