The House of Favourite Newspapers

Masau Bwire Afunguka Simba Walivyompa Ofa

0

WAKATI jina la Masau Bwire, Ofisa Habari wa Ruvu Shooting likitajwa kuibukia mitaa ya Msimbazi kubeba mikoba ya Haji Manara, kiongozi huyo amefungukia namna mabosi wa Simba walivyompa ofa ili awe ndani ya kikosi hicho.

 

Kwa sasa nafasi ya Ofisa Habari wa Simba ipo mikononi mwa Ezekiel Kamwaga ambaye anakaimu na aliweka wazi kuwa atasepa hivi karibuni kwa kuwa mchakato wa kumtafuta mbadala wake unaendelea.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Masau alisema kuwa, Simba walimfuata zamani ili awe kwenye kitengo cha usemaji lakini alikataa kwa kuwa roho wa Bwana hakumpa ruhusa kufanya hivyo.

 

“Kuna vitu viwili unaweza kuvichanganya, kwamba mimi pengine nafurahia kwenda kufanya kazi Simba, kama ningekuwa napenda kufanya hivyo ningefanya kazi siku nyingi sana kwa sababu Simba waliwahi kunifuata ili nikafanye kazi pale.

 

“Simba waliwahi kunihitaji siku nyingi tena kwa nguvu lakini bado roho wa Bwana alikuwa hajaruhusu, walinifuata sana nilikataa, ilikuwa zama za utawala wa Aveva (Evans) na Kaburu (Godfrey Nyange) pengine ningekubali mimi, Manara (Haji) asingekuwepo pale.

 

“Walinifuatilia sana kwa kujua kwamba Hassan Hasanoo (Othuman) alikuwa ni rafiki yangu na ana ushawishi kwangu basi wakasema amesema nikamsalimie wakati huo alikuwa mahabusu ila lengo ilikuwa ni kumtumia yeye anishawishi ili niweze kufanya kazi katika klabu hiyo, nilisimamia msimamo.

 

“Sio Simba tu hata Wananchi yaani Yanga walinifuata, niliwaambia kwamba sipo tayari hata kipindi cha Charles Mkwasa alipokuwa katibu nilifuatwa lakini bado roho wa Bwana hakuruhusu.

 

“Pia Azam FC wamenifuata, nakumbuka walinifuata mara tatu na kuna wakati walinifuata Uwanja wa Taifa kipindi hicho kwa sasa ni Uwanja wa Mkapa, niliwashirikisha waandishi wengine ikiwa ni pamoja na marehemu Kashasha, ila nilibaki kuwa na msimamo wangu.

 

“Sifurahii kwamba sasa nachukuliwa kwenda kufanya kazi huko ila furaha yangu ni namna ambavyo watu wananitazama. Sifanyi kazi kwa kufikiria kikija kitu chenyewe maamuzi yangu yatafanyika hapo. Siwezi kutoa maoni katika kitu ambacho hakipo,” alisema Masau.

RICHARD NGAILLA NA LUNYAMADZO MLYUKA

Leave A Reply