The House of Favourite Newspapers

MASHA: NAKUBALIANA NA KATIBA ILIYOPO

0

MASHA: NAKUBALIANA NA KATIBA

 

KADA mkubwa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Lawrence Masha amesema hana shida kabisa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyopo sasa huku akiwataka watu waache kupotosha umma kuhusu jambo hilo. Akichangia mjadala kwenye Kongamano la Meza ya Uzalendo, Jumamosi ya wiki iliyopita ndani ya Ukumbi wa Nkurumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Masha ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alisema haoni ubaya wala kasoro za katiba hiyo na kwamba jambo muhimu la kufanya ni kuhakikisha watu wanakuwa wazalendo kwa nchi yao kuanzia viongozi na raia wa kawaida.

 

Akizungumza kwa kujiamini, mwanasiasa huyo aliyewahi kushika nafasi ya uwaziri wa mambo ya ndani na ubunge wa Nyamagana, Mwanza aliweka wazi kuwa endapo kila mwananchi atakuwa mzalendo kwa taifa lake, yaani viongozi kutimiza majukumu yao kwa moyo wa kizalendo na wananchi wanafanya yaliyo upande wao kwa kujitoa kikamilifu kwa taifa, hakuna sababu za kulaumu na kukosoa katiba iliyopo na kwamba hata kama itatungwa nyingine mpya yenye uzuri wa kila aina, kama hakuna uzalendo wa kweli ni kazi bure.

 

“Binafsi sioni kabisa tatizo ya katiba iliyopo, unajua muhimu sana ni kuwa na uzalendo wa kweli kwa taifa letu, mimi ni mwanasheria kitaaluma na nyote hapa mnajua, naisoma katiba yetu vizuri sana na haina shida, msisitizo ni kuwa na uzalendo kuanzia kwa viongozi na raia wa kada zote kwa kuipenda sana nchi yetu, kujifunza mambo mengi yanayohusu taifa letu leo.

 

“Ni aibu kama nyinyi nyote hapa hamumjui mtu kama Mti Mkavu au Black Mamba, tatizo tulilonalo sisi Watanzania ni kukosa uzalendo na kutopenda kujifunza kwa dhati mambo yanayohusu taifa letu, mtu asipotoshe kuwa katiba ina ubaya,” alisema Masha.

 

Aidha, kwa upande mwingine, Masha alionesha hisia za wazi kukerwa na kitendo cha baadhi ya watu kumuita mpinzani kwa sababu ya kutofautiana kimawazo kuhusu namna ya kuijenga nchi na kwamba anamtambua na kumheshimu Rais Dk. John Magufuli kama rais na kiongozi wa taifa.

 

“Hakuna kitu kinanikera kama kuitwa mpinzani, nakereka sana kwa kweli, tofauti zetu za kivyama na mambo ya mtazamo wa namna ya kuijenga nchi yetu hakumaanishi mimi ni mpinzani, namheshimu Rais Magufuli na yeye ndiye kiongozi wa taifa langu kwa sasa, tuacheni kuvurugwa na utofauti wa vyama, sisi sote ni Watanzania na tuwe na uzalendo kwa taifa letu kwa kufanya yaliyo mema,” alisema Dk. Masha.

 

 

Leave A Reply