Mashindano ya Azam Vitasa Plus Yazinduliwa Kwa Mbwembwe Dar
MASHINDANO ya michezo ya kujihami, Kung Fu, Wushu, Judo na mingineyo yaliyopewa jina la Vitasa Plus leo yamezinduliwa kwa mbwembwe baada ya wapiganaji hao kuvamia ulingo na kuanza kutesti mitambo kwa kuoneshana mikwara. Februari 6 mwaka huu mashindano hayo yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo Wakala wa Michezo kutoka China na mmoja wa waratibu wa mashindano hayo, Fu Guodong amesema ameamua kuyaamsha mashindano hayo hapa nchini baada ya kuona hamasha ya mchezo huo ilivyo juu hapa nchini.
Fu amesema mashindano hayo yataendeshwa na Watanzania lakini siku zijazo wanatarajia kuyafikisha mashindano hayo katika levo za kimataifa.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo Katibu wa Chama cha Wuchu hapa nchini, Sempay Gora Kapipi amewaasa wachezaji wa mchezo huo kujitokeza na kuushiriki kwakuwa nafasi za ushiriki bado zipo.
Sempay Kapipi amesema michezo hiyo ni ajira kama zilivyo ajira zingine na kusema kuwa washiriki wa mashindano hayo watajishindia zawadi mbalimbali.
Afisa Uhusiano wa Baraza la Michezo nchini (BMT) Frank Mgunga amewapongeza Azam TV ambao ndiyo wadhamini wakuu wa mashindano hayo ya Vitasa Plus ambayo ni mapya hapa nchini na kusema kufanya hivyo ni kuiinua michezo hiyo hapa nchini.