The House of Favourite Newspapers

Masikhara ya Dk. Mollel Yanavyompa Wakati Mgumu Elvis – Siha

0

 

Wana Siha huu si wakati wa kuongea lugha ya vyama, bali ni wakati wa kuweka mustakabali wa jimbo lenu mbele.

Dk. Mollel ni nani?

Majina yake kamili ni Godwin Mollel, huyu ni mgombea ubunge kupitia CCM. Alizaliwa tarehe 22/10/1979 kwa sasa ana miaka 40 tu. Dk. Mollel moja ya sifa yake kubwa akiwa mdogo, ni uwezo wake kitaaluma na uchangamfu.

Hapo zamani kutokana na uhaba wa shule za sekondari, wanafunzi wengi walikuwa hawapati nafasi za kujiunga na Shule za Serikali na zamani shule za kata zilikuwa hazipo, hivyo aliyekuwa anakwenda sekondari hizi za boarding, walikuwa wale waliofaulu sana darasani, na ukipangwa shule kama Kibaha, Ilboru, Mzumbe na Tabora Boys kwa wavulana, basi mwanafunzi huyo alikuwa kipanga kweli kweli darasani.

Dk. Mollel ni mojawapo ya wanafunzi wachache waliowahi kuvunja mwiko huo wa kuaminishwa kuwa wanafunzi hawafaulu na aliacha maajabu pale shule ya msingi Magadini kwa kufaulu sana na kupangwa shule ya Sekondari Kibaha. Hii ni sifa ambayo kila ukikutana na mwalimu wake, lazima aizungumzie.

Dk. Mollel Kitaaluma ni daktari aliyehitimu 2007 shahada ya kwanza pale Muhimbili hivyo huyu kama si siasa, angelikuwa yupo hospitalini anashughulika na wagonjwa.

Na katika kazi zake kama daktari, amewahi kufikia cheo cha kuwa RMO (Regional Medical Officer) kwa sasa ni naibu waziri wa afya.

Pia katika utumishi wake kama daktari, aliwahi kuwa mkuu wa hospital ya Siliani Arusha na aliwasaidia kufanikisha kuwaondolea kero ya deni la shilingi bilioni moja, kitu ambacho kiliwafanya kanisa la Kilutheri Tanzania kumpatia nishani maalumu.

Amelifanyia nini jimbo lake na Siha kwa ujumla?

Kwa haraka haraka, kama si mtafiti ukiona Dk. Mollel anavyochangia bungeni, unaweza kudhani ni mtu wa masikhara mengi. Ila kama utawekeza kwenye kutafiti nini alichokifanya jimboni kwake, basi utagundua kuwa huyu jamaa pamoja na kuwa genious wa darasa, lakini kwenye ubunifu na kusukuma agenda, ni bora sana.

Kama ukifanya survey ya majimbo ya Mkoa wa Kilimanjaro, Jimbo ambalo mbunge kafanya kazi kubwa, basi Dk. Mollel ataongoza. Haya ni baadhi ya mambo aliyoyafanya:

Akiwa kama mbunge, amewezesha kuibana Serikali yake na Siha ikanufaika na ujenzi wa kilomita 73 za barabara ambazo zimegharimu zaidi ya shilingi milioni 142. Hakuna jimbo ambalo limefanikiwa kupata kiwango kikubwa cha fedha kama hizi toka Serikalini kwa ajili ya kujenga barabara.

Kwenye hospitali ya Kibong’oto na wana Siha ni mashahidi, pale kuna ujenzi unaendelea nje ya geti la hospitali, jengo lile la ghorofa ni kwa ajili ya maabara ya kisasa ya kuchunguza ugonjwa wa TB Tanzania. Lile jengo mpaka sasa limeshatafuna bilioni tisa na kazi inaendelea.

Amesukuma agenda ya upanuzi wa hospitali ya wilaya na umefanyika upanuzi mkubwa uliogharimu bilioni mbili, lakini pia hospitali imepata mashine ya X-ray yenye thamani ya shilingi milioni 250.

Amefanikisha ujenzi wa mabweni ya shule kwenye jimbo lake, ambayo mabweni hayo yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 332 na akaipandisha hadhi shule ya Namwai na kuwa Advance. Mwabweni haya ni mkombozi mkubwa hasa kwa watoto wa kike.

Wana Siha ni mashahidi, katika kipindi chake amezindua miradi 12 ya maji ya uhakika. Kwa kutaja mifano tu mradi wa lawati fuka na Magadi Makiwaro, ni mfano wa kazi alizofanya Dk. Mollel.

Amefanikisha kusukuma agenda ya kujengewa madaraja  yanayounganisha kata za Kashashi na Ivaen madaraja mawili yenye tahamani ya shilingi milioni 960 kila moja.

Katika Kipindi chake hicho hicho, bilioni 5.5 zilitengwa na Tarura wilaya kushughulikia sehemu zote zenye barabara korofi na ambazo hazipotiki.

Kata za Levish, Ivaen na Kashashi ni mashahidi Dk. Mollel amefanikisha kuchonga barabara zote za kata hiyo kwa kutumia milioni 840. Huku kata za Bariri na Karansi zikitumia milioni 660.

Alipoingia madarakani, alikuta ndani ya jimbo lake umeme ukiwa umefika vijiji 28 tu. Katika kipindi cha miaka mitano, amefanikisha vijiji 32 kufikiwa na umeme. Hii ina maana kuwa kati ya vitongoji 166 vya jimbo zima, vimebakia vitongoji 23 tu kila kitongoji kipate umeme. Hii ni kasi ya ajabu haijawahi kutokea Siha.

Dk. Mollel amefanya mengi pale Siha, ila moja ambalo limenigusa nikiwa hapa Siha, ni kusikia kuwa kwa kutumia mshahara wake, anasomesha wanafunzi 107 katika shule tofauti tofauti. Wanafunzi hawa hawatoki tu Siha, bali wanatoka kila pembe ya nchi hii, na wanasoma kwenye shule mbalimbali.

Je, Elvis Mosi atamuweza Dk. Mollel?

Hili swali nimejiuliza sana nikamwangalia Elvis Mosi pamoja na kwamba sijazisikia kazi zake sana, ila kwa aina ya siasa tulizonazo sasa, ungeniambia nimshauri Elvis, ningemwambia kama kweli anawapenda watu wa Siha, aache Mollel asonge mbele.

Binafsi si muumini wa propaganda, nikiwa hapa Siha wanasema ukimchagua Elvis hutomuona, kwani mara nyingi yupo Morogoro akishughulika na biashara zake. Mimi kwangu hili si la maana sana kwenye mizani za nani achaguliwe kati ya Mollel na Elvis Mosi.

Wana Siha wekeni kwenye mizani hili na mtafakari kwa kina kabla ya kuamua kupiga kura. Nimekuwa mkweli siku zote na hata viongozi wakuu wa nchi, wanayarudia haya kila siku kuwa baadhi ya majimbo walichagua vibaya. Sserikali ya CCM kwa dhahiri na wazi kabisa, imeamua kuwapa kipaumbele wabunge wake kwanza.

Keki ya Taifa haitoshelezi kwa kila kitu, hivyo kile kidogo kinachopatikana wanakigawa kwanza kwa wabunge wao. Litakuwa ni kosa kubwa kama hamjasoma mchezo.

Ikumbukwe kuwa, sasa Siha imeanza kuchora ramani ya kujipambanua kutoka kwenye wilaya duni Mkoani Kilimanjaro na kuwa Wilaya bora kabisa.

Kupanga ni kuchagua, aidha mchague maendeleo au mchague porojo za miaka mitano. Wakati wenzenu watakapokuwa wananufaika, ninyi msilalamike mkae kimya hivyo hivyo.

Yangu ni hayo, naondoka hapa Siha. NA THADEI OLE MUSHI –0712702602.

Leave A Reply